TTCL

EQUITY

Wednesday, October 9, 2013

Elimu ya Siasa na Sayansi ya Jamii

ELIMUni tendo au uzoefu wenye athari ya kujenga akili, tabia ama uwezo wa kimaumbile wa mtu binafsi. Katika dhana ya kiufundi, elimu ni njia ambayo hutumiwa kimakusudi na jamii kupitisha maarifa, ujuzi na maadili kutoka kwa kizazi kimoja hadi kingine.
 
Haki ya kusoma imeweza kuelezwa kuwa haki ya kimsingi ya binadamu katika kifungu cha pili cha itifaki ya kwanza ya maagano ya haki za binadamu barani Ulaya kuanzia mwaka wa 1952 ambapo wanachama wote wanashurutishwa kuhakikisha elimu kwa wote. Katika kiwango cha kimataifa, Mapatano ya Umoja wa Mataifa ya haki za kiuchumi, kijamii na utamaduni katika mwaka wa 1966 yanahakikisha haki hii katika kifungu cha 13. Wanafunzi ama vijana waliopo vyuoni ama shuleni pia wanahitajika kujua umuhimu wa wao kuwa ni sehemu ya jamii ya uongozi katika familia, jumuiya mbalimbali na pia kwenye mamlaka za taifa na kimataifa. Hayo ndiyo matokeo ya elimu yanayohitajika. Elimu ya sayansi ya jamii ni somo muhimu linalounganisha jamii bila kujali rangi, kabila ama elimu yao, hivyo wasomi wanalo jukumu la kuiunganisha jamii si kujitenga na jamii tena kwa kujenga kuta ndefu kuzingira nyumba zao!. Hivyo elimu ya shosholojia ni muhimu kuzingatiwa miongoni mwa wasomi. Sosholojia ya elimu ni somo linalohusu jinsi taasisi za kijamii huathiri michakato na matokeo ya elimu, na kinyume chake. Kwa wengi, elimu hueleweka kama mbinu ya kushinda vizuizi, kufanikisha usawa na kupata amani na hadhi kwa wote (Sargent 1994). Wanafunzi wanaweza kutiwa motisha na tamaa ya maendeleo na uboreshaji. Elimu hutambuliwa kama mahali ambapo watoto huweza kujikuza kulingana na mahitaji yao ya kipekee. Jukumu la elimu laweza kuwa ni kukuza mtu binafsi hadi kilele. Uelewa wa shabaha na mbinu za michakato ya utangamano wa kielimu hutofautiana kulingana na dhana ya sosholojia iliyotumika Hali kadhalika kwa wasomi wenye malengo ya kuwa viongozi katika mamlaka ama taasisi mbalimbali sharti watambue elimu ya sayansi ya jamii ni sehemu ya weledi katika uongozi, ingawa kiongozi si yule tu mwenye madaraka, bali sifa ya kiongozi ni kuongoza wengine katika njia sahihi. Mwanafalsafa Plato anaamini katika kanuni yake kwamba binadamu aliumbwa kuishi kijamii na wengine wanaamini jukumu kubwa la taifa ni kuundwa kwa Serikali sahihi na kamili lenye raia wake itakayowahakikishia amani na usalama katika maisha yao ya hapa duniani na ya mbinguni pia. Mintarafu ya uongozi katika taifa lolote sharti kiongozi mkuu na mwenye sifa za kutawala awe: “mwenye busara na uwezo wa kutumia akili yake vizuri sana, mwenye kumbukumbu sahihi ya mambo, mwenye uwezo mkubwa wa kueleza mambo, asiyerukia mambo na kutoa maamuzi bila kutafiti, mwenye kujirudi na kushaurika, mkarimu na mpole kwa raia wake, mpenda kutenda na kutendewa haki, mwenye msimamo na asiye dhaifu katika kutekeleza maamuzi au maazimio yaliyokubalika.” Kama akikosekana mtu mmoja mwenye sifa hizo zote, hapo itabidi watafutwe watu wawili au watatu au wengi zaidi, ambao kwa pamoja, kutokana na sifa za mmoja mmoja, wanaweza kuzikamilisha na hivyo wapewe dhamana ya kuunda Serikali ya Taifa hilo. Hapo zamani kabla ya kuwepo kwa somo la Sosholojia (sociology) kama lijulikanavyo hivi leo, kabla hata ya maelezo ya akina Comte, Vico, Marx na Spengler, inaelezwa kulikuwepo na watalaamu wengine ambao walishaelezea historia, na hatua za maendeleo ya jamii ya wanadamu, na walijaribu kutoa maelezo ya kina kuhusu umuhimu wa somo la Historia na maendeleo yake kwa siku zijazo. Kwa kweli, ni kazi yenye maelezo kuhusu mambo mengi na yaliyoelezwa kifasaha ambapo historia yenyewe imeelezewa kuwa ni sehemu ya somo la Falsafa kwa maneno yafuatayo: “Hebu tutazame undani wa somo la Historia”, anasema Ibn Khaldun na kwamba; ‘’ni uchunguzi na uthibitisho wa taarifa, uchunguzi makini wa sababu za kuwepo kwa mambo (kama yalivyo) na werevu wa kina wa jinsi mambo yalivyoweza kutokea. Hivyo, Historia ni mojawapo ya sehemu za somo la Falsafa, na inapaswa kutambuliwa kama mojawapo ya elimu ya sayansi.” Hii ndiyo dhana ya kileo juu ya somo la Historia, kutokana na kuona umuhimu na nafasi yake katika uchambuzi wa taarifa mbalimbali na kutafuta chanzo au sababu za mambo. Historia inapaswa kuwa ni elimu ya kudumu katika ustaarabu wa mwanadamu na saikolojia yake. Ni vigumu kuweza kuchambua kwa kina kazi kubwa waliyoifanya baadhi ya wachambuzi ama waandishi wa historia na kwamba huenda si mambo yote yalipata nafasi ya kuhifadhiwa katika kumbukumbu. Chunguzi za uadilifu juu ya upoteaji na uharibifu wa staarabu mbalimbali, katika mzunguko, na mchango mkuu wa wasomi katika uundaji wa mataifa mbalimbali. Kujitambua na kutambua mambo kwa ajili ya mafundisho ya kizazi kijacho ndio mwenendo muhimu uliotiliwa maanani na wasomi wa ‘kale’ kama ambavyo wasomi wa sasa wanavyotakiwa kuwa mfano wa mazao bora kwa msaada wa akili kwa wengine. Mmoja wa wasomi na waandishi wa historia alipindukia pale alipoainisha maisha ya taifa lolote na ya watu au ya kiumbe kingine chochote, kwamba hata mataifa yanazaliwa, yanakua na yanakufa. Pia kwamba mataifa yako chini ya kanuni ya mabadiliko asilia. Ibn Khaldun anatajwa ni mmoja wa wahusika na uvumbuzi wa kanuni hii ya mabadiliko ya taifa lolote. Mawazo yake ya kiuchumi kama ya kisiasa, yameendelea kutumika hata leo. Mwandishi huyu kutoka iliyokuwa ikiitwa Maghreb (Morocco) anasema: “Taifa ni sawa na mfanyabiashara mkubwa, kwani ana jukumu la kuhakikisha kuwa pesa azipatazo kutokana na kodi, zinarudi na kuwazungukia watu. Kodi za wastani ni motisha tosha ili watu waweze kujituma katika kufanya kazi. Kwa upande mwingine, kupandisha kodi yoyote tena kiholela holela, kunaweza kusababisha yasipatikane mafanikio ya malengo ya kodi husika.” Hivyo elimu ya siasa na sayansi ya jamii haviwezi kutenganishwa, kwakuwa siasa inahusu watu miongoni mwa watu na sayansi ya jamii ni ule uhusiano wa jamii yenyewe katika mambo mbalimbali ya kimaisha, kwa sababu hiyo ni muhimu kwa wanafunzi kuelewa baada ya kuwa wanafunzi wanatakiwa kuishi kwa sura ipi kadri ya viwango vyao vya elimu, lakini vyenye matokeo ya elimu ya kuishi kijamii.

No comments:

Post a Comment