Chama cha Alliance For Democratic Change (ADC) Kumeibuka mgogoro mzito ndani ya Chama cha Alliance
For Democratic Change (ADC), baada ya Bodi ya Wadhamini kuisimamisha
kamati tendaji ya chama hicho.
Kamati hiyo inajumuisha viongozi wote wakiongozwa na Mwenyekiti wa
chama hicho, Said Miraaj, huku viongozi hao wakisema hawatambuiuamuzi
huo wa bodi. Akizungumza na Nipashe, jijini Dar es Salaam juzi,
Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya ADC, Kimangale Ayubu Mussa, alisema
imeamua kunyang`anya maamlaka ya viongozi hao kwa sababu Katiba ya chama
kifungu cha 72 na 73 kinawaruhusu kufanya hivyo baada ya kuona
wameshindwa kuwajibika ipasavyo. Alisema moja ya sababu ya kuisimamisha
kamati hiyo ni kushindwa kuwajibika katika uchaguzi mkuu uliopita na
kusababisha chama kupata matokeo mabaya na kuambulia patupu hata katika
viti vya udiwani.
Mussa alisema sababu nyingine ni kamati hiyo ikiongozwa na
mwenyekiti wa chama iliandika barua kwenda Tume ya Taifa ya Uchaguzi
(NEC) ya kutosimamisha mawakala katika uchaguzi huo bila ya
kuishirikisha bodi hiyo, jambo ambalo hawakuridhishwa nalo kwa sababu
viongozi hao walipaswa kufanya hivyo kutokana na kusimamisha mgombe
urais.
Alisema wakati wowote watatangaza uongozi wa muda ambao utafanya
kazi mpaka uchunguzi wa kuchagua viongozi wengine utakapofanyika.
Alisema Katiba ya chama hicho inaruhuru bodi kuteua viongozi wa muda
iwapo waliokuwa wakishikilia nafasi hizo wataondolewa na kwamba uteuzi
unatakiwa kufanyika ndani ya kipindi kisichozidi mwezi mmoja. Hata
hivyo, alisema uchunguzi juu ya tuhuma zinazowakabili viongozi hao
utakapokamilika, kama kuna atakayekutwa hana hatia ataendelea na nafasi
yake na watakaokutwa na hatia watawajibishwa.
Alitaja nafasi ambazo ziko wazi baada ya viongozi hao kusimamishwa
kuwa ni, mwenyekiti wa chama taifa, makamu mwenyekiti, katibu mkuu,
naibu katibu mkuu na nafasi zote za wakurugenzi.
Akizungumzia uamuzi huo wa bodi, Miraaj alisema hawatambui uamuzi
huo na wao bado ni viongozi halali kwa sababu haina mamlaka ya kufanya
hivyo.
Alisema juzi walipeleka malalamiko yao kwa msajili wa vyama vya siasa ya kupinga uamuzi huo wa bodi.
No comments:
Post a Comment