TTCL

EQUITY

Thursday, June 27, 2013

TRA;KODI ZILIPWE KWA MTANDAO

Kodi ya magari kulipwa kwa simu


Dar es Salaam. Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), imesema inaanzisha mfumo wa wamiliki wa magari kulipia leseni za magari kwa kutumia simu za mkononi, ili kuondoa foleni katika ofisi za mamlaka hiyo.
Hayo yalisemwa jana na Mkurugenzi wa Fedha wa TRA, Saleh Mshoro, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kuanzishwa kwa mfumo mpya wa ulipaji kodi kwa njia ya mtandao utakaoanza rasmi Julai mosi mwaka huu.
Mshoro alisema kumekuwa na msongamano wa walipaji wa leseni hizo kwa sababu ni benki chache zinazotumika katika malipo ya kodi hiyo.
“Kuanzia mwezi ujao wateja wetu watakuwa wakilipia leseni hizo kwa kutumia simu za mkononi kwa kutuma namba ya gari lake TRA ili aweze kuelezwa anatakiwa alipe shilingi ngapi halafu atalipa kiasi hicho kwa njia ya simu na kisha kwenda kwenye ofisi za TRA kuchukua leseni yake,” alisema.
Alisema benki zote zilizopo nchini zitaingizwa katika mfumo huo ili kurahisisha ulipaji na kuondoa foleni zilizopo hivi sasa.
Akizungumzia mfumo wa kulipa kodi kwa njia ya mtandao, Mshoro alisema utatumika kwa wafanyabiashara ambao hulipa kuanzia Sh5 milioni na kuendelea.
Alisema kwa wale wanaolipa chini ya hapo wataendelea kutumia mfumo wa sasa.
“Utaratibu huu utarahisisha ulipaji wa kodi na kupatikana kwa taarifa mbalimbali za kodi kwa haraka,” alisema Mshoro.
Mshoro alisema mlipaji kodi atalipia katika benki yoyote na taarifa hizo zitafika TRA kwa haraka hivyo kurahisisha ufanyaji wa biashara za wateja wao.
Alisema mfumo huo umefanyiwa majaribio kwa miezi sita na kuonekana unafaa na wameshirikiana na Benki Kuu ya Tanzania katika kufanikisha utaratibu huo.
Alielezea matumaini kuwa wamiliki wa magari kote nchini, watafurahia mfumo huo.

No comments:

Post a Comment