TTCL

EQUITY

Wednesday, February 15, 2017

Mvutano wajitokeza saa chache kabla ya mazungumzo kuanza mjini Arusha

Mazungumzo baina ya Burundi yalizinduliwa rasmi nchini Uganda Jumatatu, Desemba 28, kupitia upatanishi wa rais wa Uganda, Yoweri Kaguta Museveni.
Mwezeshaji katika mgogoro wa Burundi, Benjamin Mkapa, anatazamiwa kujaribu tena kuleta pamoja serikali na upinzani kwenye meza moja ya mazungumzo kuanzia Alhamisi hadi Jumamosi wiki hii mjini Arusha (kaskazini mwa Tanzania), mchakato ambao unaonekana kutozaa matunda yoyote.
Rais mstaafu wa Tanzania anataka kujadiliwa kwa mara ya kwanza "masuala nyeti", kama vile muhula wa tatu wa Rais Pierre Nkurunziza unaoendelea kuzua utata na "uundwaji wa serikali ya umoja wa kitaifa," amesema mwanadiplomasia wa Afrika ambaye hakutaka jina lake litajwe.
Rais mstaafu wa Tanzania amealika katika mazungumzo hayo "kundi la watu 33 kwa upande wa serikali na washirika wake, na upande mwengine wanasiasa wa upinzani," amesema mwanadiplomasia huyo.

 
Mazungumzo baina ya Burundi yalzinduliwa rasmi nchini Uganda, Desemba 28, 2016.
 
Mkapa amewaalika hasa viongozi wakuu wa muungano wa wanasiasa walio uhamishoni na ndani ya nchi (Cnared), ikiwa ni pamoja na kiongozi wake Jean Minani, pamoja na vigogo wa zamani wa chama tawala cha CNDD-FDD ambao wanaishi uhamishoni baada kupinga muhula wa tatu wa Rais Nkurunziza.
Hata hivyo, majaribio ya kuwaleta kwenye meza moja ya mazungumzo serikali ya Burundi na upinzani walio uhamishoni hadi sasa yameshindwa. Serikali ya Bujumbura imekataa mpaka sasa kuketi kwenye meza ya mazungumzo na Cnared licha ya shinikizo na vikwazo kutoka jumuiya ya kimataifa.
"Cnared vuguvugu ambalo halitambuliwi na sheria ya Burundi na linaundwa na watu wanaotafutwa na vyombo vya sheria vya Burundi," Willy Nyamitwe, Mshari Mkuu wa mawasiliano wa rais ameliambia shirika la habari la AFP.
"Kwa hiyo ni wazi kwamba kuwaalika katika mchakato wowote wa mazungumzo ni tusi ambalo haliwezi kamwe kukubaliwa na serikali," Willy Nyamitwe amesema na kuongeza kuwa serikali ya Bujumbura itakataa kuketi kwenye meza ya mazungumzo na Cnared au mpatanishi wa Umoja wa Mataifa kwa Burundi Jamal Benomar.
Cnared kwa upandeimetangaza kuwa haitoshiriki katika kikao hicho cha mazungumzo.
Muungano huo wa wanasiasa wa upinzani ulimkataa Benjamin Mkapa kama mwezeshaji wa mgogoro wa Burundi, baada ya kusema mwezi Desemba kuwa haifai kuendelea kupinga "uhalali" wa kuchaguliwa kwa mara nyingine tena Rais Pierre Nkurunziza.
Cnared, ambayo inabaini kwamba katiba ya Burundi haimruhusu Nkurunziza kuwania muhula wa tatu, hata hivyo, "itatuma ujumbe wake kwenda mjini Arusha kuonana na Mkapa na kupata maelezo kadhaa kabla ya kuchukua uamuzi wa mwisho wa kushiriki au la katika mazungumzo hayo, " amesema mmoja wa viongozi wake, ambaye hakutaka jina lake litajwe.
Hayo yakijiri asasi za kiraia zaidi ya 11 nchini Burundi zimetoa wito kwa serikali ya Bujumbura, kutoshiriki kwenye mazungumzo ya amani ya Arusha, yaliyoandaliwa na mratibu wa mazungumzo hayo, rais wa zamani wa Tanzania Benjamini Mkapa, kwa kile asasi hizo zinasema ni kualikwa kwa upande unaotuhumiwa kushiriki katika jaribio la mapinduzi mwezi April 2015.
Burundi imetumbukia katika mgogoro mkubwa tangu mwezi Aprili 2015 pale Rais Pierre Nkurunziza alipotangaza nia yake ya kuwania muhula wa tatu na kuchaguliwa kwa mara nyingine tena mwezi Julai mwaka huo huo. Machafuko nchini Burundi yamesababisha vifo vya zaidi ya watu 500 na watu zaidi ya 300,000 kukimbilia nje ya nchi.

No comments:

Post a Comment