TTCL

EQUITY

Wednesday, February 15, 2017

Kama Unampenda kwa Dhati, Huwezi Kushindwa Kumsamehe

Ni matumaini yangu kwamba msomaji wangu uko poa! Leo utakuwa nami Rammy Gallis nataka kuzungumza nawe msomaji kuhusu ishu ya msamaha. Penzi la kweli husamehe! Yawezekana kauli hiyo ikawa nyepesi sana kuitamka mdomoni lakini ni wachache wenye moyo wa kuitekeleza.
Tunashuhudia katika maisha yetu ya kila siku jinsi watu waliowahi kupendana kwa dhati au wanandoa walioishi kwa furaha kwa muda mrefu wakiachana kwa vurugu na ugomvi kwa sababu ya mmoja wao au wote wawili kushindwa kusameheana na kufungua ukurasa mpya katika mapenzi yao.
Takwimu zisizo rasmi zinaonesha kuwa zaidi ya nusu ya wanandoa wanasalitiana na kati ya hao ni wachache mno huweza kuendelea na uhusiano baada ya kugundua kuwa wamesalitiwa na wenzi wao.
Zipo sababu nyingi zinazosababisha usaliti lakini lengo langu leo siyo kuzungumzia hilo bali ni kujaribu kuiponya mioyo ya wanandoa au watu wanaoishi kwenye uhusiano wa kimapenzi, waliojeruhiwa na usaliti.
Yawezekana ulitokea kumpenda sana mwenzi wako, ukaamini wewe ndiyo kila kitu kwake, ukamtimizia kila kilichokuwa ndani ya uwezo wako lakini mwisho, ukaambulia maumivu baada ya kugundua kuwa anakusaliti.
Vitabu mbalimbali vya dini vinaeleza kuwa kosa pekee linaloweza kuivunja ndoa, hata ile iliyofungwa kwa baraka za Mungu, iwe ni madhabahuni au msikitini, ni USALITI.
Sitaki kupingana na maandiko hayo lakini nataka tujadiliane, ni lazima kila unapogundua kuwa mwenzi wako amekusaliti dawa yake ni kupeana talaka au kuachana kwa ugomvi? Dunia imebadilika, wanaume wengi wanasaliti ndoa zao kwa sababu moja au nyingine, hali kadhalika wanawake.
Mathalani umefunga ndoa na kuishi na mwenzi wako kwa kipindi kirefu mkipendana, kujaliana na kuoneshana kila aina ya mahaba lakini akateleza na kukusaliti ilihali bado anakupenda, utakapoamua kuachana naye na kwenda kwa mwingine, ukigundua naye anakusaliti utafanya nini? Utaachana na wangapi? Utaolewa na kuachika mara ngapi?
Bila shaka umeanza kunielewa kwamba siyo mara zote talaka au kuachana ndiyo suluhisho la usaliti ndani ya ndoa. La hasha! Siwafundishi watu wasaliti ndoa zao au uhusiano wao kwa makusudi wakitegemea kusamehewa, hapana.
Ninachotaka kukijengea hoja ni kwamba, hata baada ya mwenzi wako kukusaliti, bado mna nafasi ya kuendelea na maisha yenu ikiwa tu mtaamua kulishughulikia tatizo hilo kwa kina bila kujali watu wa nje wanasemaje.
Usikilize moyo wako, ni kweli amekusaliti! Amekuumiza, unahisi dunia yote imekuelemea, unatamani kufa au kuua, lakini je, moyo wako unakuambia nini? Upo tayari kumruhusu mwizi wako ndiye awe mmiliki halali wa mwenzi wako ambaye umetumia muda mrefu kumjenga awe vile unavyotaka?
Jibu sahihi halitapatikana kwa kukurupuka, hakuna uamuzi wa busara unaotoka ukiwa na hasira, jazba au ukiwa na shinikizo kubwa kutoka kwa marafiki, ndugu, majirani na watu wanaokuzunguka.
Pata muda wa kurelax kisha usikilize moyo wako, majibu yatakayotoka ukiwa umetulia, ndiyo yatakayoamua kama uendelee au usiendelee na uhusiano uliosababisha ukaumia.
Yawezekana wewe ndiyo ulikuwa sababu ya mwenzako kuchepuka, au ni tamaa za kimwili ndizo zilizomsukuma kuyafanya hayo, lakini jambo la msingi ni kujiuliza; bado anakupenda? Anaonesha kujutia makosa yake? Anakiri na kukuomba msamaha? Kabla hajakusaliti, mmefanya mambo mangapi mazuri? Tuliza akili kisha amua.
Wanachokosea watu wengi, inapotokea ugomvi ndani ya nyumba au katika uhusiano wa mapenzi, wengi huweka vinyongo na matokeo yake, vinyongo hivyo hukua taratibu na siku matatizo yakitokea tena, ukichanganya na vinbyongo vya muda mrefu ambavyo mtu anakuwa amevihifadhi, matokeo yake hasira zinakuwa kali mara dufu na mtu anashindwa kabisa kusamehe, hata kama ni tatizo dogo limetokea.
Ushauri wa msingi, inapotokea mwenzi wako amekukosea na akakuomba msamaha, msamehe kwa moyo wote na siyo kuweka vinyongo moyoni. Na wewe unapomkosea mwenzako, muombe msamaha nausirudie makosa. Kwa namna hiyo, itakuwa ni rahisi kukusamehe.

No comments:

Post a Comment