TTCL

EQUITY

Wednesday, January 13, 2016

Mtandao wa Wanawake wa Katiba wampa neno Magufuli.

Rais Dk. John Magufuli.
 
 Mtandao wa Wanawake wa Katiba na Uchaguzi chini ya uratibu wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), umemtaka Rais Dk. John Magufuli, kuzingatia usawa katika uteuzi uliobaki ili kuleta mabadiliko chanya katika serikali ya awamu ya tano.
 
Baadhi ya nafasi zilizosalia mpaka sasa ni uteuzi wa wabunge, mabalozi, wakuu wa mikoa na wilaya, wakuu wa taasisi na mashirika ya umma pamoja na wajumbe wa bodi.
 
Mkurugenzi Mtendaji TGNP, Lilian Liundi, aliyasema hayo wakati akitoa maoni yake kuhusu uteuzi uliofanywa na Rais Magufuli kwamba haukuzingatia usawa wa jinsia kulingana na Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2015/20.
 
Liundi alisema serikali ya awamu ya tano hajaonyesha mwanzo namna ya kutekeleza Ilani ya chama tawala kama inayoelekeza kwa kumuwezesha mwanamke kushika nafasi sawa na mwanaume kwa maana ya asilimia 50/50 katika uongozi kwenye vyombo vya maamuzi ngazi zote.
 
“Tunasisitiza kuheshimiwa na kutekelezwa kwa vitendo kwa malengo hayo ili wanawake wapate fursa sawa za kutoa maamuzi juu ya masuala muhimu ya taifa letu, tunaitaka serikali kutekeleza ahadi zake za kuzingatia usawa wa kijinsia kama ilivyoainishwa kwenye Ilani ya CCM,” alisema Liundi.
 
Aidha, alimtaka Rais Dk. Magufuli na viongozi wenzake, kusimamia kikamilifu utekelezwaji wa mikataba mbalimbali iliyosainiwa na Tanzania hususan ile inayohusu usawa wa kijinsia ili kupunguza pengo lililopo.
 
Liundi aliitaja mikataba hiyo kuwa ni pamoja na Mpango Kazi wa Beijing wa mwaka 1995, Mkataba wa Maputo, Mkataba wa Nyongeza wa Jinsia na Maendeleo Kusini mwa Afrika na tamko la Umoja wa Mataifa la Haki za Binadamu (1948).

No comments:

Post a Comment