Mhe. Freeman Mbowe mwenyekiti wa chama cha demokrasia na maendeleo CHADEMA.
Ujumbe huo ulibebwa katika moja ya mabango na mwananchi mmoja
wakati wa maadhimisho ya miaka 52 ya Mapinduzi Zanzibar yaliyofanyika
katika Uwanja wa Amaan mjini Unguja jana.
Katika taarifa za vyama hivyo vyenye upinzani mkubwa wa kisiasa
nchini, kwa nyakati tofauti zimeelezea kusikitishwa na ujumbe huo.
Kwa upande wake, Chadema kimesema kwa namna bango lenye ujumbe huo,
ni vigumu kuamini kuwa liliibuka ghafla kama vile kitambaa cha mfukoni.
Hayo yamo katika taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari jana jioni na chama hicho kupitia Idara ya Mawasiliano na Habari.
Viongozi wakuu wa Chadema akiwamo Mwenyekiti wake, Freeman Mbowe,
Kurugenzi za chama, watendaji na wataalam wake, wamejichimbia mkoani
Kilimanjaro kwa siku kadhaa sasa wakiendelea na vikao vya tathmini na
uchambuzi ambao kwa kawaida hufanyika kila mwanzo wa mwaka, vikiitwa
'retreats'
"Chadema tunalaani na kupinga kwa nguvu zote mabango, mikakati,
tabia na chembechembe za ubaguzi wa aina yeyote, ukiwamo huu wa kisiasa
ambao sasa unaanza kusakafiwa na kwa sababu hiyo, tunaamini wanaobeba
ajenda hii hawataishia hapo," ilisema sehemu ya taarifa hiyo na
kuongeza:
"Bali watazidi kutugawa Watanzania. Chadema kwa kusimamia misingi
yake na kuzingatia kikamilifu misingi ya taifa letu hasa haki, uadilifu,
utu, umoja na uzalendo; haiko tayari kuona taifa likihatarisha maisha
ya jamii kwa sababu ya kikundi cha maslahi ya watu wachache."
Imeongeza wakati taifa na chama hicho vikimtakia Rais,Dk. John
Magufuli, afya njema na nguvu ya kutimiza kwa vitendo kauli yake ya kuwa
serikali yake haitawabagua watu kwa misingi ya kisiasa, ni vyema
serikali ikachukua hatua kuwawajibisha viongozi waliosimamia na kuachia
jambo hilo kutokea huko Zanzibar.
Aidha, Chadema kimemkumbusha Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Ernest
Mangu, kwamba kauli za namna hiyo zisipodhibitiwa ni hatari kwa amani
ya nchi na usalama wa raia na mali zao.
CCM kwa upande wake, imesem, imesikitishwa na ujumbe huo wenye maudhui ya ubaguzi.
Taarifa iliyotolewa na Mkuu wa Mawasiliano na Umma CCM, Daniel Chongolo, ilieleza kuwa Chama kinaomba radhi kwa ujumbe huo.
Ilisema CCM inapinga na kukemea kabisa fikra, hisia na mitazamo yoyote yenye maudhui ya kibaguzi kupitia ujumbe huo.
“Ujumbe huo siyo tu kuwa una maudhui ya kibaguzi, bali pia
unakwenda kinyume kabisa na falsafa na shabaha ya waasisi wa Mapinduzi
Matukufu ya mwaka 1964 na unapingana na misingi, itikadi ya CCM
inayohimiza umoja na mshikamano wa kitaifa,” ilisema sehemu ya taarifa
hiyo.
KARUME AZOMEWA
Na katika hatua nyingine, Rais mstaafu wa Zanzibar, Dk. Amani Abeid
Karume, alizomewa na baadhi ya wananchi wakati akiingia na akiondoka
katika Uwanja wa Amaan mjini Unguja wakati wa maahadhimisho hayo jana.
Tukio hilo lilitokea siku moja tangu Umoja wa Vijana wa Chama Cha
Mapinduzi (UVCCM) kukitaka chama hicho kimfukuze uanachama kwa madai
amekuwa akishirikiana na wapinzani kuzorotesha malengo ya CCM visiwani
Zanzibar.
Kitendo cha kuzomewa kiongozi huyo kilianza kujitokeza wakati
viongozi wa kitaifa wakiwasili uwanjani na kutangazwa na mshereheshaji
mtangazaji wa zamani wa Sauti ya Tanzania Zanzibar, Suleiman Juma Kimea.
Hata hivyo, baada ya kulitaja jina la Dk. Karume, watu waliokuwa
wamekaa katika jukwaa la karibu na viongozi wa kitaifa walianza kupaza
sauti zao za zomeazomea...“huyooo…msaliti huyooo… msaliti, hatumtaki.
Walisikika wakipiga kelele watu hao wengi wao wakiwa na sare za CCM.
Dk. Karume aliendelea na itifaki ya kuwasalimia viongozi wa kitaifa
kabla ya kukaa katika kiti, lakini hali hiyo iliendelea kujitokeza tena
wakati Rais huyo mstaafu akiondoka uwanjani baada ya kukamilika wa
sherehe hizo.
Wakati hayo yakitokea, Dk. Karume alionekana akinyanyua mikono na
kuwapungia kama ishara ya kuwasalimia waliokuwa wakifanya vitendo hivyo.
Mkasa huo ulitokea siku moja baada ya Mwenyekiti wa Umoja UVCCM,
Sadif Khamis Juma, kukitaka chama kimvue uanachama Dk. Karume kama
walivyofukuzwa wanachama wengine baada ya kwenda kinyume na miko na
maadili ya chama hicho.
Akihutubia katika mkutano wa hadhara katika maahadhimisho ya miaka
52 ya Mapinduzi ya Zanzibar katika Uwanja wa Maisara juzi, alidai kuwa
Karume amekuwa akishirikiana na wapinzani kuimaliza CCM kisiasa
Zanzibar.
“Tunakitaka chama chetu kuchukua hatua muhimu kama zile
zilizochukuliwa mwaka 1987, kilipowavua uanachama akiwamo aliyekuwa
Waziri Kiongozi Seif Sharif Hamad na wenzake sita, akafuatia Mansoor
Yussuf Himid, Hassan Nassor Moyo na sasa tunataka afukuzwe mara moja
Amani Abeid Karume,” alisema Sadif katika mkutano uliohudhuriwa na Rais
wa Zanzibar Dk. Shein.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar,
Mohamed Aboud Mohamed, alipoulizwa alisema hawezi kuzungumzia mkasa wa
Dk. Karume kuzomewa.
"Siwezi kuzungumza chochote, Karume alikuwa bosi wangu nyie kama
waandishi ndiyo mnatakiwa kuwauliza waliofanya kitendo hicho wamefanya
kwa sababu gani,” alisema Waziri Aboud.
Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inamheshimu Karume kama
Rais mstaafu na kumpa sitahiki zote zinazotakiwa kwa mujibu wa sheria.
No comments:
Post a Comment