TTCL

EQUITY

Friday, December 4, 2015

RC kujadili magendo ya sukari

Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Amos Makalla.
 MKUU wa Mkoa wa Kilimanjaro, Amos Makalla amesema anatarajia kuzungumza na uongozi wa mkoa wa Tanga na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kudhibiti matumizi mabaya ya bandari na uingizwaji sukari kutoka nje ya nchi kwa njia za panya.
Licha ya sukari hiyo kutajwa kutishia uhai wa viwanda vya ndani vinavyozalisha bidhaa husika, Makalla alisema, uingizaji holela unainyima serikali mapato na hivyo kuathiri ukuaji uchumi wa taifa kwa ujumla.
Makalla alisema hayo juzi wakati akijibu taarifa ya Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kiwanda cha Sukari cha TPC Ltd, Robert Baisac aliyekuwa akielezea mafanikio na changamoto zinazowakabili tangu mwaka 2000.
“Hili la sukari kutoka nje kuingia kwa njia za panya halikubaliki, tutatumia vyombo vyetu vya ulinzi na usalama ili kulidhibiti mapema kabla athari hazijawa kubwa zaidi,”alisema. Alishutumu watumishi wasio waaminifu katika bandari ya Tanga kwa kushirikiana na wafanyabiashara, ambao wanadaiwa kuingiza shehena za sukari kutoka nje ya nchi na hivyo kuua soko la ndani.
“Lazima serikali mkoani Kilimanjaro itafanya mazungumzo na wenzetu wa Tanga ili kuziba matumizi mabaya ya bandari...hii isipodhibitiwa mapema, tutajinyima mapato lakini pia tunamkatisha tamaa mwekezaji ambaye ameweka mtaji wake wa mabilioni ya fedha,” alisema.
Makalla alisema serikali imetengeneza mazingira rafiki kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi sanjari na ushindani wa biashara, lakini si sukari ya nje kuingia nchini kwa njia za panya na kutolipiwa kodi.
Katika taarifa yake kwa Mkuu wa Mkoa, Baisac alisema pamoja na juhudi kubwa zilizofanywa katika uwekezaji, kiwanda kinakabiliwa na ushindani usio sawa baina ya sukari wanayozalisha na inayoingizwa kutoka nje ya nchi.
Alisema mahitaji ya sukari kwa taifa kwa mwaka ni takribani tani 400,000 lakini kiasi kinachozalishwa na viwanda vya ndani ni tani 320,000. Alishauri iwapo upo ulazima wa kuingia kwa sukari kutoka nje, lazima ifuate utaratibu uliowekwa badala ya kuingizwa kwa njia zisizo rasmi.

No comments:

Post a Comment