TTCL

EQUITY

Wednesday, November 11, 2015

Sera Ya Vijana, Kwa Ajili Yako

 Image result for vijana
UNAFAHAMU kwamba kuna Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana ambayo ilitengenezwa kwa ajili ya kuwatengenezea vijana mazingira ya kufanikiwa, kuendelea na kushiriki kwenye jamii.
Sera ya Vijana ina mapendekezo mengi mazuri. Ni wachache kati yetu ambao tunafahamu uwepo wa sera hii, kwa hiyo tumeamua kuwashirikisha wenzetu uelewa wetu juu ya baadhi ya mawazo na mapendekezo ya Sera hii ambayo yatakushawishi kuchukua hatua.
Sera ya Vijana inaunga mkono mazingira yatakayowawezesha vijana kushiriki kwenye shughuli zinazowahusu.
Mfano mzuri wa hili ni Kituo cha Jamii Kigamboni (KCC), ambacho kilianzishwa na Festo Chengula pamoja na wenzake mwaka 2006. Aliona kulikuwa hakuna kitu ambacho vijana wenzake walikuwa
wakijishughulisha. Walikuwa wanakaa tu vijiweni wakipiga soga siku nzima. Walihitaji kitu cha kufanya kwa ajili ya kupambana na umaskini na wajiepushe na tabia hatarishi!
“Kundi letu lilihitaji kufanya kitu, hivyo tulikutana na kuanzisha kituo cha jamii. Watano kati yetu walianzisha changamoto na tukatumia ujuzi wetu na uelewa wetu kwenye sanaa, kucheza muziki, michezo na masomo kuongeza nguvu kwenye klab,” alieleza Festo.
Serikali ya Mtaa ilimpa Festo na kundi lake chumba kwa ajili ya shughuli zao kwenye ofisi, wakati serikali ya mtaa ilipokuwa haina mikutano.
Vijana kadha wa kadha wakaanza kujiunga na pakachangamka! Mwaka mmoja baadaye walitengeneza katiba ya klab, ambayo ilifuatiwa na kusajili shirika la kijamii na wakajiunga kama Klab ya Fema.
Mara wakapewa eneo zaidi na serikali ya mtaa na baada ya muda mfupi wakapata ardhi yao binafsi. “Kikundi sasa kina ardhi yake na tunajihusisha na shughuli mbalimbali kuanzia kutengeneza cheni hadi ufundi cherehani na kucheza muziki na maigizo.
Tuna duka letu wenyewe ambapo tunauza vitu vya wanachama wa kikundi chetu, tunacheza muziki muda wowote tunaotaka. Hii inatuingizia kipato kwa wanachama,” anasema.
Festo anatamani kuona mabadiliko ya jinsi watu wazima, hasa wa serikalini wanawaangalia vijana wanaojituma kwa nguvu kutimiza malengo yao ya maendeleo. Anahisi kituo chao ni mfano mzuri wa ushirikiano kati ya vijana, Serikali yao ya Mtaa na jamii!
Kikundi cha KCC kimefanikisha kile ambacho kimetamkwa kwenye Sera ya Vijana kama nia ya kuwaandaa vijana kutimiza wajibu wao kwenye jamii, kwa mifano halisi.
Lakini hilo likifanywa...
Nini kinatokea kama vijana wanataka kujihusisha na maamuzi yanayofanywa kwenye jamii yao?
Kikundi cha waelimishaji rika kiitwacho Magu Youth Development Network (MAYODEN), cha Mwanza, kimefanya uamuzi wa kutumia mapendekezo yaliyopo kwenye Sera ya Vijana ya kuwa na utaratibu wa kuwezesha ushiriki kamili wa vijana katika mfumo wa serikali za mitaa, serikali kuu n vyombo vingine vyya ushirikishwaji katika ngazi za kitaifa na kimataifa.
Wamefanikiwa kuwa na wawakilishi wa vijana kwenye vyombo vya maamuzi.
“Kundi letu lina wajumbe wawili kwenye ngazi ya wilaya na mmoja ngazi ya kata ambao wanawakilisha kikundi chetu na vijana wengine kwenye Serikali ya Mtaa.” Anaeleza Mwenyekiti wa MAYODEN, Victor Sadalah (32).
Sera ya Vijana inasema kwamba kuwe na raslimali za kuwawezesha vijana kiuchumi.
“MAYODEN Tunatoa mikopo kutoka kwenye fedha tunazopata kutoka kwa wadau mbalimbali ambao waliamua kutusadia baada ya kuona jinsi gani tunajitoa.
“Hatukai tu na kusubiri fedha kutoka kwa Serikali, kwa sababu tukifanya hivyo tutasubiri kwa muda mrefu! Pia tunajitahidi kukuza utamaduni wetu, kupitia ngoma za asili na uigizaji, hili linasaidia kuwaepusha wasichana na majanga.”
MAYODEN imethibitisha kwamba vijana wanaweza kuaminiwa, na kusaidia katika maendeleo na kuhamasika hata katika ngazi ya wilaya.
Fema Clubbers wamo pia...
Sera ya Vijana inapendekeza kuwe na mazingira yanayohimiza ongezeko la ushiriki wa vijana kwenye shughuli za kujitolea.
Shule za sekondari za Lindi na Kawawa, zilizopo Mufindi, Iringa, zimetoa muda kwa wanafunzi kushiriki shughuli za kujitolea!
Wanafunzi wanawatembelea wagonjwa hospitalini, kama wanawake wajawazito na kujaribu kuwasaidia kwa kuwapa mahitaji mbalimbalia kama sabuni, dawa za mswaki, biskuti na maneno ya kutia moyo.
“Tunahimiza sana kujitolea. Pale wajumbe wa klabu wakiwa na muda wa ziada, wanaweza hata kufanya usafi kwenye bwalo la hospitali.” Alieleza Mlezi wa Fema Club, katika Shule ya Sekondari Kawawa, Frank Mwaimu.
Tuifanye Sera ya Vijana itufaidishe
Sera ya Vijana ilitengenezwa kwa lengo la kufanya maisha yawe mazuri kwa vijana wa Tanzania. Hata hivyo, tunatakiwa kushiriki kupitia mipango yetu wenyewe kama tunataka mambo yaende mbele.
Huu ni ushauri kidogo kwa ajili yako.
  • Kuwa na taarifa kuhusu kile unachoweza kufanya kusaidia maendeleo yako binafsi na ya jamii nzima inayokuzunguka.
  • Vijana wana haki ya kuwa na wawakilishi kwenye serikali ya kijiji, kata, na wilaya. Wawakilishi hao ndio watu wa kuwaona kama una swali au dukuduku lolote na wanatakiwa wapeleke maoni yako kwenye vikao.
  • Fahamu uamuzi unaofanywa na wawakilishi wa jamii yako. Changamka, jihusishe kwenye mambo yanayokuzunguka!
Jifunze kutoka kwa vijana wengine wa Tanzania ambao wameonyesha kwamba penye nia pana njia!

No comments:

Post a Comment