TTCL

EQUITY

Sunday, July 7, 2013

NGURUWE WAPIGWA MARUFUKU JIJI LA ARUSHA

 HOMA YA NGURUWE  KATIKA JIJI LA ARUSHA

Nguruwe ni kitoweo kinacho pendwa na watu hasa kwa ladha, ulaini wa nyama yake nyeupe (white meat) ambapo baadhi ya watu hushauriwa na wataalam kuitumia nyama hii kwa sababu haina lehemu (cholestral) na mafuta yake hayagandi mwilini hivyo utumiaji wa nyama hii hunguza uwezekano wa kuugua magonjwa mbalimbali. Aidha mnyama huyu ambaye kuishi kwake hakutegemei gharama kubwa idadi yake imekuwa ikiongezeka siku hadi siku.
Hivi karibuni idara ya Kilimo, Mifugo na Ushirika Jijini Arusha imeeleza kuwepo kwa virusi hatari wanaosababisha homa ya nguruwe (African swine fever).
 akielezea kwakina Daktari wa mifugo Jiji la Arusha. Andronicus N. semufali amesema kuwa eneo lote la jiji la Arusha na wakazi wote hawaruhusiwa kuchinja, kuingiza au kutoa wanyama jamii ya nguruwe katika maeneo ya Jiji bila kibali cha maandishi cha Daktari wa Mifugo.
Aidha ugonjwa huu wa homa ya nguruwe (African swine fever) ni ugonjwa wa homa ya nguruwe unaoenea kwa kasi na kuuwa hata nguruwe wote wanaoambukizwa. Ugonjwa huu unasababishwa na virusi na hauna chanjo ya kuukinga.
Virusi hivi vinaishi ndani ya nguruwe pori bila madhara yoyote, Kupe aina fulani wanapomng’ata na kunyonya damu kutoka kwa nguruwe pori wanabeba virusi hivi. Kupe hawa wanatoa mazingira mazuri ya uzalishaji wa virusi vingi na kuviingiza kwenye nguruwe wanaofugwa mara kupe hao wanapomng’ata nguruwe afugwaye.
Baadaya hapo virusi ndani ya nguruwe anayefugwa huzaliana kwa kasi na kwa maumbile tofauti huku virusi vikisababisha ugonjwa wa homa ya nguruwe. Uambukizaji kati ya nguruwe wafugwao hauhitaji kupe bali kugusana ama nguruwe kula mabaki ya nguruwe aliyechinjwa ama maji maji yatokanayo kwa nguruwe anayeumwa
Imeelezwa kuwa virusi vya homa ya nguruwe havijaonesha kuwa na madhara yoyote kwa binadamu wala wanyama wengine wafugwao, isipokuwa muonekano wa nyama ya nguruwe aliye athirika na virusi (African swine fever) haina muonekano  mzuri na nyama yake haina ladha.
Virusi vya ugonjwa huu Jijini Arusha vilithibitishwa kuwepo mwezi juni 2013, baadaya nguruwe kuonekana kufa na wengine kuwa walegevu katika eneo la Dampo lililopo Kata ya Sokon 1 na Terati. Kwa sababu nguruwe hao huachiwa na Wafugaji kuzurura katika eneo hilo wakijitafutia chakula ndipo walipokula mabaki ya Nguruwe waliosafirishwa kutoka Wilaya ya Rombo na kuchinjwa hapa Jijini Arusha na mabaki yake kutupwa eneo hilo la Dampo.
Katika vipimo vya awali vilivyopelekwa kitengo cha magonjwa ya mlipuko na baadaye kupelekwa Chuo Kikuu cha Kilimo (SUA) imegundulika kuwepo kwa virusi hivi. Utafiti wa awali uliofanyika, Virusi hivi vimebainika kuwa vimeanzia Wilaya ya Rombo Mkoani Kilimanjaro.
Aidha Dr. Andronicus alieleza kuwa kuchinjwa kwa Nguruwe aliye athirika na virusi, na mabaki yake kuachwa, kama vile mifupa na manyoya yake kuzagaa bila ya kufukiwa ama kuchomwa kunasababisha kuendelea kusambaa kwa ugonjwa wa homa ya nguruwe. Uchunguzi wa awali umeendelea kuonesha kuwa nguruwe aliye athiriwa na virusi hivi uwezekano wake wa kuishi ni mdogo kwani ugonjwa huu unaua kwa kasi. Pia kwa mtu yeyote akimshika nguruwe aliyeathirika na baadaye kumshika ambaye hakuathirika bila ya kunawa ni rahisi kumwambukiza.
Kitaalamu imeonesha kuwa sio virusi vyote vyenye madhara, kila mnyama huwa na virusi vyake. Virusi hivi ni vya nguruwe tu na havina madhara kwa binadamu wala wanyama wengine.
Dalili za homa ya nguruwe ni pamoja na Homa kali, weusi na wekundu sehemu zisizo na manyoya mengi kama vile masikio, sehemu za tumbo na miguu. Ugonjwa huu unaweza kusababisha vifo mpaka asilimia 100 ndani ya saa 24. Nguruwe anaacha kula kabisa, nguruwe anashindwa kutembea vizuri na kupenda kulala chini muda wote.
Hakuna tiba yoyote ya ugonjwa wa homa ya nguruwe. Pia hakuna taarifa zozote za kuwepo kwa chanjo ya kinga kutokana na kwamba kirusi kinachosababisha ugonjwa huu kinabadilika badilika na ni sugu kuweza kuishi kwenye joto la kawaida kwa zaidi ya miezi 18.
Uongozi wa Jiji la Arusha umechukua hatua za awali kuweka karantini kuzuia kusafirisha nje ama kuingiza nguruwe au mazao yake ili kuzuia ugonjwa usienee zaidi ndani ya Jiji, Wilaya, Mkoa na Nchi za Jirani. Pia kuuwa na kuzika nguruwe wote walioathirika, mabaki ama mazao yake yatokanayo na nguruwe walioambukizwa.
Hata hivyo umezuia ulishaji wa nguruwe kutokana na mabaki ya nguruwe waliochinjwa, na kutahadharisha Wafugaji nguruwe waliokaribu na mapori yaliyo na nguruwe pori kuwaogesha nguruwe kuzuia kupe, kuzuia nguruwe wafugwao kwenda kupata malisho kwenye mapori yaliyo na nguruwe pori, kutochukuwa malisho ya nguruwe wafugwao kutoka maeneo yaliyo na nguruwe pori.
Sababu za kuweka karantini ni kutekeleza sheria ya kuzuia magonjwa ya mlipuko kwa mujibu wa sheria za nchi ya Tanzania. Sheria ya kuzuia ugonjwa huu kimataifa unahimiza hivyo pia. Aidha daktari wa mifugo atakayezembea kuzuia kuenea kwa ugonjwa huu katika wilaya yake atakuwa amefanya kosa dhidi ya taaluma yake. Kwakufanya hivyo atawajibishwa na chombo kinachosimamia fani ya udaktari wa mifugo Tanzania.
Ugonjwa umeshawahi kuenea kutoka Afrika kwenda mabara mengine mara mbili kuanzia mwaka 1957. Ugonjwa ulitokea nchini Kenya kwa mara ya kwanza kati ya mwaka 1909 na 1915 na kusababisha vifo vya asilimia (98.8%) ya nguruwe wote walioambukizwa.  Mwaka 1933 ulitokea afrika ya kusini na kusababisha vifo asilimia (92%) ya nguruwenwote walioambukizwa.
Ni jukumu letu sote kama Wananchi wa Jiji la Arusha kuzuia kuenea kwa ugonjwa huu ambao unasababisha hasara kubwa kiuchumi kwa watu binafsi, familia na taifa lote kwa ujumla.
Chanzo cha habari na; Daktari wa Mifugo Jiji la Arusha Androci N. semufali pamoja na Afisa habari Jiji la Arusha Ntegenjwa Hosea.
Angalizo: Ewe Mtanzania mwenzangu mpenzi msomaji na mshirika wa blog hii nijukumu langu mimi na wewe kama Watanzania kuzingatia Agizo hili la serikali kuhakikisha ugonjwa huu hauendelei kuenea, tuchukue hatua kupinga usafirishaji na uchinjaji usiozingatia vigezo.

No comments:

Post a Comment