TTCL

EQUITY

Sunday, June 5, 2016

Usikubali kovu lizuie mafanikio mbele yako


 


UNAPOKUWA na kovu au makovu ni ushahidi kuwa palikua na kidonda, kwa sababu ni hali ya kawaida kidonda kuacha kovu ingawa hutofautiana ukubwa kulingana na ukubwa wa kidonda.

Makovu mengine hupotea baada ya siku kadhaa, mengine wiki, miezi, mengine huchukua miaka kupotea na kuna mengine hayapotei kabisa yanabaki siku zote. Kawaida kovu halina maumivu, kama kuna maumivu basi bado ni kidonda na hakijapona, kovu huwa kama kumbukumbu tu lakini isiyo na maumivu.
Kuna sababu nyingi zinazoleta vidonda vinavyoacha makovu. Kuna makovu yanayoachwa na vidonda vilivyopatikana katika kujifunza, kujifunza vitu kama vile wakati wa utoto unapojifunza kutembea ukaanguka na kuumia, unapojifunza kuendesha baiskeli na mafunzo mengine. Bila kujifunza huwezi kufahamu na katika kujifunza unakutana na vidonda vinavyoacha makovu.
Makovu mengine yanapatikana katika kufanya yale unayopaswa kufanya kama vile katika kazi unazofanya mfano kupika ukaungua, unajenga nyumba ukaumia na kuna makovu yanapatikana kutokana na kusababishwa na watu wengine, kusukumwa ukaumia, kupigwa na mambo yanayofanana na hayo na mwisho makovu yatokanayo na vidonda ulivyopata wakati unamsaidia mtu.
Vidonda vya makovu haya yote vinauma, lakini kuna ambavyo maumivu yanaishia mwilini na mengine yanaingia hadi rohoni, katika maisha yetu ya kawaida pia tunakutana na kuumia kwingi, kunakoacha makovu ya aina mbalimbali. Makovu mengine unayasahau baada ya muda mfupi, lakini mengine hayaondoki kabisa.
Unaweza kuumizwa unapotafuta kazi ukatendewa jambo ambalo likakuumiza sana lakini baada ya kupata kazi ukasahau kabisa, au ukaumia katika masomo yako, hali ikawa mbaya lakini unapokuja kumaliza na kufaulu unasahau yote.
Lakini kuna maumivu hasa ya kutendwa na mtu wa karibu sana kama mchumba, kutengwa na ndugu, kuachwa baada ya kuvalishwa pete, kutendwa na mume au mke, kufukuzwa kazi bila kosa na mengine ya aina hiyo ambayo mara nyingi hukaa muda mrefu au hayaishi kabisa.
Katika haya yote unapaswa kuzingatia kuwa kovu halina maumivu. Litakuwepo pale kukukumbusha kuwa ulipitia haya na sasa umevuka, kukuonya kuwa usipite mahali fulani utaumia na kukutia moyo kuwa yamepita na sasa ni mshindi na kwa imani tunasema umeshinda na zaidi ya kushinda.
Kumbuka kovu halina maumivu ila ni kumbukumbu na si kizuizi katika maisha yako, ingawa wapo watu wanaamini kutumia makovu kama kizingiti ama kizuizi katika maisha yao. Nasema hivi kwa kuwa kuna ushahidi wa baadhi ya watu ambao wameamua wenyewe kuacha makovu yawe vizingiti vya kuwazuia kusonga mbele na kama kovu hilo ni maumivu, basi linadhihirisha kuwa kidonda hakijapona.
Si siri wapo watu wamepitia machungu na maumivu makali sana katika maisha yao, ambayo kiuhalisia wameachwa na makovu makali ambayo kwa akili na uwezo wa kibinadamu, hayawezi kufutika na hivyo yanakuwa ni kizingiti miaka na maisha yote. Unapofikia katika hatua hii, sijui imani yako ni nini?
Lakini nasema unapofikia katika hatua hii ya kuendelea kuwa na kovu lisilopona, basi mgeukie Mungu kwani ndio tabibu wa kweli akuponye kidonda na kuondoa maumivu yote.
Kumbuka kidonda kilichopona kovu haliumi, kwa sababu kovu halioneshi kesho yako itakuwaje ila linaonesha nyuma ulipitia nini, usikubali kuwa mfungwa ama mtumwa wa makovu kwa sababu ukiruhusu hivyo umejiwekea vizingiti vya kusongambele.

No comments:

Post a Comment