TTCL

EQUITY

Tuesday, May 17, 2016

Undani wa Mauaji ya Watu 7 Sengerem

Na Johnson James,
MWANZA: Vilio, majonzi, simanzi na sintofahamu bado vimetawala kwenye Kitongoji cha Nyigumba, Kijiji cha Sima wilayani Sengerema kufuatia watu saba kwenye nyumba moja kuuawa kwa kukatwakatwa mapanga na binadamu wenzao wasio na utu.
Tukio hilo ambalo bado ni bichi, lilijiri Mei 11, mwaka huu kwenye nyumba ya marehemu hao iliyopo jirani na Shule ya Msingi Sima.

WALIOPOTEZA MAISHA
Watu hao saba waliopoteza maisha ni Eugenia Philipo Kwitega, 60, (pichani)  ambaye alikuwa mama mwenye nyumba, Maria Philipo Kwitega (50) ambaye ni mdogo wa mama mwenye nyumba, Mabula Makeja (20), yeye alikuwa mwanafunzi wa kidato cha nne na Mkiwa Philipo Kwitega (12), mtoto wa Eugenia aliyekuwa akisoma Shule ya Msingi Sima.

Mauaji Sengerema (10)
Wengine ni Leonard Aloyce (13) aliyekuwa mwanafunzi wa Shule ya Msingi Sima, Donald (40) na Samson (23) ambao walikuwa wafanyakazi katika familia hiyo. Wao miili yao ilisafirishwa kupelekwa wilayani Ngara, Kagera kwa mazishi.

Mauaji Sengerema (19)

mwandishi wetu alifunga safari hadi kijijini hapo ili kupata mkasa mzima kwa kina, na kushuhudia miili hiyo ikizikwa kijijini hapo, alizungumza na msemaji wa familia hiyo ambaye ni mtoto wa marehemu Eugenia, baadhi ya majirani na ndugu wengine.

Mauaji Sengerema (18)

TETESI ZA MITAANI
Patrick Joshua ambaye ni msemaji wa familia, alisema tetesi zilizozagaa mitaani baada ya vifo hivyo kwamba familia hiyo ilikuwa ikichukiwa na baadhi ya watu, si za kweli kwa vile mama yake alikuwa akishirikiana na watu wote katika kijiji hicho na waliishi kwa furaha na amani.

Mauaji Sengerema (16) 
WIVU WA MAENDELEO WATAJWA
Baadhi ya watu msibani hapo walisikika wakisema wanaamini waliotekeleza mauaji hayo walikuwa na wivu wa maendeleo yaliyopo kwenye familia hiyo.
Walisema mpaka mauaji hayo yanatokea, marehemu Eugenia alikuwa amepiga rangi nyumba yake, umeme upo muda wote, ana ng’ombe wa maziwa wasiopungua kumi na tano na mbuzi ishirini.

Mauaji Sengerema (15)“Unajua marehemu aliajiri wafanyakazi kutoka Kagera kuja kufanya kazi za shambani na mifugo, hicho si kitu kidogo. Naamini wivu wa maendeleo umewasukuma watu kuimaliza hii familia.

Mauaji Sengerema (9) 
“Maisha ya marehemu Eugenia yalikuwa bora hapa kijijini, maadui hawakupenda. Ndiyo maana hata walipoingia, walianza kutaka pesa kwanza, walipokosa ndiyo wakaamua kuua,” mwombolezaji mmoja alisikika akimwambia mwenzake.

Mauaji Sengerema (20) 
UTABIRI WA JIONI YA SIKU YA TUKIO
Mtu mmoja alilsema kwamba jioni ya usiku wa tukio, hali kwenye nyumba hiyo ilikuwa ya kupooza kama vile kulikuwa na ubashiri wa tukio.

Mauaji Sengerema (14) 
“Mimi nilikatiza mida ya jioni, nikadhani Eugenia ameondoka kwani nyumba nzima ilikuwa kimya wakati si kawaida. Mama mwenye nyumba alikuwa mtu wa kucheka na watu muda wote.

Mauaji Sengerema (5) 
“Lakini pia usiku wa kama saa mbili hivi, nikasikia ng’ombe wakilia kama vile wameingiliwa na kitu kibaya, baadaye wakanyamaza. Sasa kuja kusikia familia imekatwakatwa mapanga, nikaanza kuamini kuwa kulikuwa na roho ya utabiri ila haikujulikana,” alisema mwananchi mmoja bila kutaja jina lake.

Mauaji Sengerema (17) 
WALICHOSEMA WALIONUSURIKA
Kwa mujibu wa mtoto wa marehemu Eugenia, Patrick, watoto walionusurika kukatwa mapanga katika tukio hilo kwa kujificha chini ya uvungu wa kitanda walisema siku ya tukio, saa nane usiku wakati wamelala, watu wawili wakiwa na mapanga walifika nyumbani hapo na kuulizia pesa.
“Wanasema walipozikosa pesa, ndipo wakaanza kumshambulia Donald. Lakini Donald alipambana nao sana ila kwa bahati mbaya akateleza, wakamshinda nguvu na kuanza kumkatakata mapanga.

Mauaji Sengerema (6) 
“Wakati hayo yakiendelea, mama mwenye nyumba akatoka na kwenda kufungua mlango wa chumba walicholala wajukuu zake, ndipo watu hao nao wakaingia na kuanza kutekeleza unyama huo kwa kuwashambulia wote kwa mapanga.”

JIRANI ASIMULIA
Kulwa Lusoloja ambaye ni jirani wa familia hiyo, alisema: “Nilipata taarifa ya vifo hivyo saa 12 asubuhi kutoka kwa ndugu wa marehemu, akaniambia kuwa kwenye familia ya Eugenia kuna msiba mkubwa umetokea, watu saba wameuawa kikatili kwa kukatwakatwa mapanga akiwemo mama mwenye nyumba. Nilitoka kwenda na kukuta maiti moja nje ikiwa imetapakaa damu. Inauma sana.”

WALIONUSURIKA WAHIFADHIWA POLISI
Kwa mujibu wa msemaji huyo, vijana hao walionusurika (majina tunayo) wanahifadhiwa na Polisi Sengerema ili kuwanusuru na njama zozote za watu hao kutaka kuwamaliza kwa vile inadaiwa kuwa walizitambua sauti za wauaji hao.

ALICHOSEMA RPC WA MWANZA
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, ACP Ahmed Msangi alisema kuwa uchunguzi bado unaendelea kuhakikisha wote waliohusika na mauaji hayo wanatiwa mbaroni ili sheria ifuate mkondo wake.

Mauaji Sengerema (8) 
MAJIRANI WAISHI KWA HOFU
Baada ya tukio hilo, baadhi ya majirani waliozungumza na mwandishi wetu na kusema wanaishi kwa hofu kwa vile wanahisi hata wao wanaweza kuvamiwa wakati wowote na kuuawa. Hata hivyo, polisi wameweka ulinzi mkali eneo hilo.
“Kwa kweli hata sisi majirani sasa tunaishi kwa wasiwasi, hofu yetu ni kwamba watakuja kutukata hata sisi kwani kama waliweza kuwakata wale wa familia nzima watashindwa nini kutukata na sisi?” alisema Fitina Likenza, mkazi wa kijiji hicho.

VIONGOZI WA DINI WATOA NENO ZITO
Wakati wa ibada iliyofanyika wakati wa kuagwa kwa marehemu hao, baadhi ya viongozi wa dini, akiwemo Askofu wa Kanisa la Africa Inland Church (AIC) Mkoa
wa Geita, Mussa Magwesela aliwaasa wananchi kumrudia Mungu kwani dunia kwa sasa imeharibika na watu wamekuwa hawaendi kwenye ibada na badala yake wanafanya mambo kinyume na maagizo ya Mungu.
Kwa upande wake, Omar Mbalamwezi aliyezungumza kwa niaba ya viongozi wa dini ya Kiislam, alidondosha machozi akisema damu ya mtu kamwe hailipiki hivyo wanadamu hawana budi kumrudia Mungu na waliofanya mauaji hayo walaaniwe.

Mauaji Sengerema (3)

MKUU WA WILAYA ATOA MOTISHA
Mara baada ya ibada hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Sengerema, Zainab Telack alisema kuwa atatoa fedha
taslimu shilingi laki mbili (200,000) kwa mtu yeyote atakayefanikisha kupatikana kwa watuhumiwa hao.
“Nitatoa fedha taslimu kwa mtu yeyote atakayetuletea taarifa za watu wanaohusika na mauaji haya, hivyo niwaombe wananchi muendelee kutuunga mkono na kushirikiana nasi ili kutokomeza vitendo viovu kama hivi katika wilaya yetu,” alisema Zainab.

NANE WASHIKILIWA
Mpaka wakati mwandishi wetu anaondoka eneo la tukio, watu nane walikuwa wakishikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza wakihusishwa na mauaji hayo.

JPM ASHTUSHWA
Mara baada ya mauaji hayo, Rais Dk. John Pombe Magufuli ‘JPM’  alilitaka jeshi la polisi kuwakamata watuhumiwa haraka huku akitoa wito kwa Watanzania kumwabudu Mungu ili kuiepusha jamii na mauaji kama hayo.

HISTORIA FUPI YA EUGENIA
Taarifa zinasema kuwa, mume wa Eugenia alifariki dunia mwaka 2008 akiwa mwalimu mstaafu. Eugenia mwenyewe pia alikuwa mwalimu na baada ya kustaafu, alipata mafao yake na kuanza miradi midogo, ukiwemo huo wa ng’ombe wa maziwa na mbuzi. Watoto wake watatu wa kiume ni wafanyakazi kwenye migodi ya dhahabu mkoani Geita.

WALIVYOZIKWA
Ukiachilia mbali marehemu wawili waliozikwa Ngara, Kagera, miili ya marehemu watano ilizikwa kwenye makaburi ya familia yaliyopo jirani na nyumba iliyotokea mauaji hayo.
Mungu azipumzishe mahali pema  roho za marehemu wote. Amina.

No comments:

Post a Comment