TTCL

EQUITY

Wednesday, January 13, 2016

Brigedia Jenerali Msuya: Serikali itakamilisha kwa haraka ukarabati wa Kituo cha Afya cha Chipole

Mkurugenzi wa Idara ya  Uratibu maafa Ofisi ya Waziri Mkuu, Brigedia Jenerali, Mbazi Msuya  ameahidi kuwa serikali itakamilisha kwa haraka ukarabati wa Kituo cha Afya cha Chipole wilayani Songea Vijijini, ambacho kinashindwa  kuhudumia wananchi elfu 7000 wa kata ya Magagura baada ya kupata majanga ya kuungua na moto mwaka 2013.

Akiongea mara baada ya kukagua shughuli za ukarabati  na kujionea hali halisi ya Kituo hicho Mkurugenzi wa Uratibu Maafa, Brigedia Jenerali, Mbazi Msuya amesema kuwa ameridhika na matumizi ya fedha za ukarabati shilingi milioni 35 ambazo zilitolewa na Ofisi hiyo na kuahidi kutoa fedha nyingine mapema mwezi huu za kukamilisha ukarabati wa kituo hicho cha Afya.
 
Kwa upande wake Afisa tabibu wa Kituo hicho,Ismail Mzimya amesema kukamilika  kwa kituo hicho kutaboresha na kuimarisha  huduma za Afya katika kata hiyo  hasa za watoto na mama wajawazito huku mmoja wa wakazi wa kata hiyo  akisema kukamilika kwa kituo hicho kutawasidia wakazi hao ambao wamekuwa wakitembea  umbali mrefu kufuata huduma za Afya na kuiomba serikali kuharakisha ukarabati wa kituo hicho cha Afya.
 
Kituo cha Afya cha Chipole kilichopo Kata ya Magagura wilayani Songea vijijini kinamilikiwa na Shirika la watawa  wa Mtakatifu Agnesi Chipole na  kinahudumia takribani wakazi 7,434  wa kata hiyo yenye vijiji 3, hivyo kukamilika kwa ukarabati wa kituo hicho  kutawezesha wakazi wa kata hiyo kuipata karibu  huduma  ya Afya.

No comments:

Post a Comment