TTCL

EQUITY

Tuesday, December 1, 2015

CDA kutambua wenye viwanja kwa kompyuta

Katikati ya Mji wa Dodoma
Katikati ya Mji wa Dodoma

MAMLAKA ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA) imeweka mfumo wa kompyuta ambao unatumika kutambua wateja wake wote wanaomiliki viwanja.
Mfumo huo ambao unafahamika kwa jina la Land Management System ambao mpaka sasa umeingiza kumbukumbu za viwanja 40000.
Akizungumzia mfumo huo, Ofisa Habari wa CDA, Angella Msimbila amesema mfumo huo unasaidia kutunza kumbukumbu za viwanja na kurahisisha mteja kuhudumiwa haraka tofauti na awali.
“Tulikuwa tukitumia muda mrefu kutafuta mafaili na tulikuwa tunakumbana na malalamiko mengi lakini baada ya mfumo huo kwa sasa huduma inaenda kasi tofauti na hapo awali,” amesema msimbila.
Ametaja mfumo mwingine kuwa ni ule wa kufunga na kufungua milango kwa kutumia kadi maalum.
Amesema mfumo huo umesaidia kupambana na madalali ambao walikuwa wakiingia ofisini hapo kiholela na kushirikiana na baadhi ya watumishi wasio waaminifu kuuza viwanja.
Angella amesema mbali na kuwepo kwa kadi maalumu za kufungua milango pia jengo zima la CDA limefungwa kamera kwa ajili ya kuwabaini wale wote ambao si waaminifu.
“Kutokana na kamera hizo unaweza kugundua mtumishi katoka ndani ya jengo na kuingia mara ngapi kwa siku na alikuwa akizungumza na nani na kwa nia ipi,” amesema Msimbila.
Wakati huohuo, CDA imetangaza mikakati rasmi ya kuufanya mji wa Dodoma kuwa kati ya mikoa bora na safi nchini tofauti na ilivyo sasa.
Mbali na kuufanya mji wa Dodoma kuwa bora CDA ilianza kutekeleza kaulimbiu ya kutunza mazingira tangu Agosti mwaka huu kwa lengo la kuufanya mji kuwa safi na wenye kuvutia.
Akizungumza na waandishi wa habari, Kaimu mkurugenzi wa CDA, Paskasi Mulagili amesema zoezi la usafi katika mkoa wa Dodoma ni endelevu na kila mtumishi ni lazima ashiriki siku huyo ya Jumamosi.
Mkuu huyo amesema mji wa Dodoma ni kati ya miji ambayo inakusudiwa kuwa jiji na ni mji ambao unapokea wageni wengi hivyo unatakiwa katika kiwango cha juu cha usafi.

No comments:

Post a Comment