Mbowe Aombe Radhi Kukubali Mwaliko wa Dhifa ya Obama
Mbowe
anatuangusha na anaangusha harakati za kuikataa CCM na serikali yake.
Lakini zaidi anatutisha sisi wengine kuhusiana na uwezo wake wa kupima
na kutumia hekima kuamua mambo. Lakini zito kabisa ni kuwa anafanya
juhudi za kuiondoa CCM madarakani ifikapo 2015 kuwa dhaifu zaidi na
hivyo kuongeza ugumu usio wa lazima kwa harakati hizo. Jambo pekee
analoweza kufanya ni kusimama na kuomba radhi wanaharakati wenzake ambao
wamefanya na kutumia muda mwingi sana kuhakikisha kuwa jamii ya
kimataifa inajua kinachoendelea Tanzania wakati wa ziara ya Obama.
Baadhi yetu tulitarajia kuwa CDM wangegongelea msumari wa mwisho wakati
wa ziara ya Obama.
Niseme
kuwa ninachosema hapa hakihusiani na Obama bali uongozi wa Mbowe katika
suala la dhifa hii. Sina tatizo na watu wengine kushiriki na kufurahia
kuonana na Obama; nina tatizo la msingi na Mwenyekiti wa CDM, chama
ambacho sasa hivi kina mgogoro na serikali na ambacho kimekuwa
kikinyanyaswa Bungeni na mikoani kuhudhuria hafla ambayo ataonekana
kukubali na kubariki serikali. Lakini zaidi kuwa kiongozi huyo kabla ya
ujio mzito wa Obama hakutoa kauli yoyote nzito ambayo ingeonesha kutaka
vyombo vya habari vya kimataifa na nchi marafiki na watu wengine wajue
kinachoendelea nchini dhidi ya upinzani, haki za binadamu na uhuru wa
maoni.
Barua ya CPJ na Makalaza za Magazeti ya Marekani
Baadhi
ya watu walishangazwa na hata kufurahishwa kwanza kuona Kamati ya
Kutetea Waandishi (Committeee for Protection of Journalists) imeandika
barua kali kwa Rais Obama kudokeza juu ya kudoda na kudorora kwa tasnia
ya uandishi huru wa habari. Barua ile ya CPJ ambayo ilitolewa nakala kwa
watu mbalimbali iliweka bayana mifano dhahiri ya jinsi dola
inavyotumika kuminya na kudumaza uandishi huru wa habari kiasi kwamba
sasa hivi uandishi unaokubalika na kuonekana ni halali ni ule usio kuwa
mkali, usiogusa serikali kwa ukali na wale usiowagusa vigogo kwa ukali.
Yaani, uandishi wa makala nyororonyororo zilizopakwa mafuta na
kupendezeshwa zisizoweza kuudhi hata kulazimisha chombo cha habari
kufungiwa.
Kutokana na hali hii mbaya ya uandishi wa habari hali imefika ambapo waandishi na vyombo vya habari vinakuwa compromised japo watawala wataonesha wingi wa vyombo vya habari kuwa ni dalili ya kukomaa kwa haki hii ya msingi ya wananchi.
Hata
hivyo barua ya CPJ haikuja hewani hivi hivi tu au kwamba hao watu wa
CPJ walikaa NY au Nairobi na wakafikiria tu labda waandike kitu tu
kutoka kwenye magazeti. Ukweli ni kuwa CPJ imekuwa ikishirikiana na
waandishi mbalimbali wa Kitanzania ndani na nje na kutuma hata watu wake
ili kufanya uchunguzi yanapotokea matukio mbalimbali.
Kwa
wale ambao hawakumbuki mwaka 2008 wakati wa ujio wa Rais Bush (Mwezi
Februari) na katikati ya sakata la Richmond Bungeni mtandao uliotangulia
huu wa JamboForums ulijikuta kwenye matatizo makubwa baada ya waasisi
wake kutiwa mbaroni na polisi kiasi cha kuhusishwa na masuala ya
ughaidi. Wengi wanaweza kuwa wamesahau lakini baadhi yetu tunakumbuka
kama vile ilikuwa jana kwani tuliweka rehani kila kitu ili kusimama
kuwatetea ndugu zetu lakini zaidi sana kutetea haki ya uhuru wa maoni.
Kwa wanaokumbuka mimi nilienda BBC Idhaa ya Kiswahili kuzungumzia hili
na kutetea uhuru wa mawazo na kusema “hata mawazo ya kijinga yana haki
kutolewa”. Lakini hatukuishia hapo, DCI Manumba na IGP Mwema
tuliwasumbua kutaka maelezo ya vijana wetu kutiwa mbaroni; hatukujali
sana kuwa kuna ugeni mkubwa nchini. Waliachiliwa bila kushtakiwa kwa
lolote.
Makala ambazo zimetoka kwenye magazeti ya Washington Post, New York Times na hata USA Today hazikutoka kwa sababu finally
vyombo hivi vimeonesha kujali kinachoendelea Tanzania. Kwamba, vyombo
hivi vikubwa hatimaye vimeamua kutokana na wema wake kumulika Tanzania.
Kufikiri hivyo ni kuwa na mawazo mafupi sana. Kuna watu wanaharakati
kwenye media na nje ya media ambao wamejitahidi kuwasiliana na hawa watu
na kuwadokeza kwa kina kinachoendelea. Hata swali ambalo Rais Kikwete
aliulizwa na mwandishi wa NBC halikutokea peponi; hivi mnafikiria mambo
ya Alan Mzengi na kesi yake ilianzia Washington Post? Au NBC? Kuna watu
wamejitahidi kumulika ukandamizaji aliofanyiwa dada Yule na zawadi
ambayo Alan Mzengi alipewa na Rais Kikwete Ikulu (wenyewe walisema ni
Mshauri wa Rais kitu si cha kweli).
Sasa
watu wanapofanya haya ili kusaidia harakati za mabadiliko wanatarajia
kuwa wale viongozi wa kisiasa na wenyewe wataonesha kuelewa cue za
wanaharakati wenzao na kuzitumia vizuri. Sasa watu wakijua kuwa macho ya
kimataifa yatakuwa Tanzania na vyombo vya habari vya kimataifa vitakuwa
vinaripoti moja kwa moja kutoka Tanzania tulitegemea viongozi wa vyama
vya upinzani na hasa CDM wangeonesha kutumia nafasi hii vizuri.
Niliandika hili mapema huko nyuma sitalirudia. Badala yake wale wale
walioenda kunywa juisi Ikulu, kusifia kazi nzuri ya CCM na serikali yake
ndio hao hao tena wameenda kuubariki utawala huu mbele ya jamii ya
kimataifa na kupoteza nafasi adhimu waliyopewa na kubebewa na wengine.
Yaani
ni kana kwamba watu wametengeneza pasi zote nzuri kuelekea golini na
hata pale golini golikipa kapigwa change na sasa ameachiwa mchezaji
nyota amalize na badala yake anaunawa mpira na kuupigapiga mabusu! Yaani
angalau angefanya kama alivyojaribu Yule Mghana Kombe la Dunia na
kupaisha kuliko kushindwa hata kujaribu! Hivi ndivyo alivyofanya Mbowe
kwa harakati. Leo hii tunaposikia wana CCM wakiibeza CDM na viongozi
wake wanafanya hivyo kwa haki kabisa!
CCM inahangaika kuidhoofisha CDM, CDM inahangaika kuiimarisha CCM?
Nimewahi
kuandika huko nyuma kuwa si jukumu la upinzani kusaidia chama tawala
kutawala. Jukumu la upinzani mahali popote duniani ni kuona chama
kilichoko madarakani (siyo serikali tu) kinadhoofika na kushindwa ili
hatimaye wananchi waamue kukikataa na kukichagua chama kingine. Hii
ndiyo dhana hasa ya upinzani. Wapinzani siyo washauri nasaha wa chama
tawala! Kwamba chama tawala kikiwa kwenye matatizo basi upinzani ndio
unakataa kusikiliza na kutoa mrejesho na baadaye watawala wanafanya
vizuri huku chama cha upinzani kinajisifia ‘tuliwapa sisi ushauri
nasaha’!
CCM
inatambua – na inatambua hili kwa muda sasa – kuwa tishio lake kubwa
zaidi ni CDM na hivyo inatumia silaha zote kutoka katika ghala lake
kuhakikisha kuwa CDM inadhoofika na kuporomoka. Nahitaji kweli kutoa
mifano juu ya hili? Kesi za kila aina dhidi ya viongozi wa upinzani,
tuhuma za ughaidi, na kunyimwa vibali vya kila namna tunaweza kusema CCM
inaipenda saaaaana CDM kiasi cha kumwalika mwenyekiti wake (nafahamu
mwaliko umetoka ‘serikalini’). Leo hii kuna tuhuma za kila namna jinsi
viongozi wa CCM wanavyowasiliana sana na watu wa serikalini ili
kuidhibiti CDM. Sasa tuseme Mbowe yeye halioni hili au halioni kwa uzito
wake?
Niliandika
huko nyuma kuwa siwalaumu kabisa CCM kujaribu kudhoofisha upinzani
nchini – hilo ndilo jukumu la chama tawala. Jukumu la chama tawala kwa
upinzani ni kuudhofisha ili usije kupata nguvu ya kukiondoa madarakani.
Ni rahisi hivyo. CCM haifanyi jambo lolote lisilo la kawaida (atypical)
la vyama vya siasa vilivyoko madarakani mahali popote. Hivi, si serikali
ya Obama hapa imejikuta na kashfa ya IRS na kashfa ya ushushu? Hiyo ya
IRS si imedaiwa kuwa IRS (Internal Revenus Service) imekuwa
ikivifuatilia kwa karibu zaidi vikundi vya kihafidhina kuliko vile vya
kiliberali? Sasa inashangaza?
Kauli za Mbowe zinatatiza harakati
Alipoamua
kusifia serikali ya Kikwete wakati wa kuweka jiwe la msingi la ujenzi
wa barabara ya Kwa Sadala Mbowe alinukuliwa kusema:
“Mimi
ni mpinzani na Mheshimiwa Rais unajua hilo, lakini wanasema ‘mnyonge
mnyongeni haki yake mpeni’. NInatembea sana ndani ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania, kwa barabara na kwa anga; na mheshimiwa Rais tunakupongeza
na mheshimiwa Waziri tunakupongeza kwa kazi kubwa sana ya kujenga
miundombinu inayofanywa ndani ya taifa letu”
Kauli
hii kwa kuiangalia kwa haraka haina tatizo lolote lile na kwa kweli mtu
atasema kuwa Mbowe alistahili kuitoa. Hata hivyo, bahati mbaya sana
imetolewa na kufanya watu wasahau kiasi cha changamoto kilivyo. Lakini
zaidi ni kusahau kuwa karibu kwenye majimbo ambayo CCM imekuwa ikipata
shida ndiko ambako pia CCM na serikali yake iko kwenye charm offensive.
Mbowe
kama kiongozi wa upinzani – na mwenyewe alisema anajijua hivyo – jukumu
lake siyo kumwaga sifa. Kama kweli Mbowe anaamini CCM na serikali yak
echini ya Kikwete inafanya kazi nzuri sana ya kujenga miundo mbinu
mbalimbali atapaswa kutuambia kwanini bado watu waitoe serikali hii
madarakani? Kwanini wawaondoe CCM kama wanafanya kazi nzuri sana hivyo
na hasa eneo la miundombinu ambalo lina mahitaji makubwa sana. Kushindwa
kuonesha kuwa kilichofanywa ni kiduchu kulinganishwa na kilichoahidiwa
ni kosa kubwa la mkakati; lakini pia kushindwa kuonesha suala la ubora
wa miundo mbinu na rushwa iliyioko katika ujenzi na ufisadi ni kosa
jingine. Ni kana kwamba kwa vile kunakojengwa ni kwao basi kafumbia
matatizo kabisa yanayoendelea nchini. Hili lilikuwa kosa ambalo
angetakiwa kuomba radhi wakati ule.
La kukubali mwaliko wa dhifa ni kosa kubwa zaidi
Sasa
hilo la kumsifia Kikwete tunaweza kuliweka pembeni na kusema kuwa
alikuwa mbele ya Mangi na yeye alitaka kuchomekea mambo mawili matatu.
Hili la Obama hata hivyo ni la makosa makubwa ya kimkakati (strategic
errors) kiasi kwamba nashindwa kuelewa kama wanazungumza na wapanga
mikakati wao au kila mmoja anajiendea kivyake vyake.
Masaa
machache kabla ya habari kuwa Mbowe amekubali mwaliko na amehudhuria
dhifa ya Obama Katibu Mkuu wa CDM Dk. Slaa akinukuliwa na gazeti la Mwananchi alinukuliwa kusema kuwa chama chake hakikupokea mwaliko wowote wa
kuhudhuria mapokezi ya Obama na hivyo wasingeenda kule. Katibu Mkuu
ndiye mtendaji Mkuu na barua za Mwaliko bila ya shaka zinaandikwa kwenda
kwake. Hivyo, wengi tulijua kuwa kama hawajapata mwaliko basi hawaendi;
siyo kususa! Unasusa pale ambapo umepata mwaliko na unaamua huendi.
Swali
kubwa ambalo baadhi ya watu wameuliza na Mbowe atapaswa kulitolea
majibu wakati wa kuomba radhi ni kuwa alipopata mwaliko wa kwenda kula
‘dina’ Ikulu alikuwa aliwasilina na Katibu Mkuu wake? Na je alijua kuwa
Katibu wake alitangaza kuwa hawakualikwa? Lakini nyuma ya hilo swali
jingine labda ni la haki zaidi ni kuwa Mbowe alipata mwaliko wa dhifa
lini? Kama aliupata mapema zaidi kabla ya Dr. Slaa kuzungumza na
mwananchi linaacha maswali mengine; kama aliupata masaa machache kabla
ya tukio lenyewe nay eye alikubali nalo linaacha maswali mengi zaidi.
Tatizo la Msingi basi ni nini?
Kwa
maneno machache ni kuwa kuna mgogoro kati ya CCM na serikali yake na
CDM. Kumekuwepo na matukio mengi yanayoonesha unyanyasaji na
ukandamizaji wa wapinzani nchini, matukio ambayo nikijaribu
kuyaorodhesha hapa itakuwa ni kurudia rudia wimbo ule ule kwa wanakwaya!
Matukio haya yameonesha wazi kabisa kuwa kuna uhasama wa kisiasa
(political animosity) kati ya CCM na CDM. Hali ambayo haijatengemaa na
kama matukio ya Arusha ni ushahidi hakuna dalili ya kutengemaa. Kesi
mbalimbali ambazo zimekuwa zikifunguliwa, vitisho na unyanyasaji wa
viongozi wa CDM ni sehemu tu ya mkakati huo wa kuidhoofisha CDM. Mbowe
mwenyewe ameshasema mara nyingi kwenye mikutano jinsi CCM na serikali
yake na vyombo vya dola vinavyowanyanyasa.
Sasa,
ama Mbowe anasema kweli kuhusu vitendo vya CCM na serikali dhidi ya CDM
au vitendo hivyo si vibaya kihivyo. Kama anasema kweli – na ninaamini
hivyo – ni jukumu lake kuhakikisha kuwa siyo tu Watanzania wanajua hili
(kwani tayari wengi wanalijua) bali jamii ya kimataifa inajua hili vile
vile. Katika kuijulisha jamii ya kimataifa hakukuwa na nafasi nzuri
zaidi ya kufanya hivyo kaa ujio wa Obama.
Wengine
wanasema alialikwa siyo kama Mwenyekiti wa CDM bali kwa sababu ni
Kiongozi wa Upinzani Bungeni (KUB); really? Na watu wenye kusema hivi
wanazungumza kabisa kama wana hekima? Kiongozi wa Upinzani wa chama gani
huko Bungeni? Na hivi huko Bungeni kuna mahusiano mazuri sana baina ya
CCM na CDM kiasi kwamba Mwenyekiti wa CCM akiandaa kitu basi KUB ni
lazima aende kwa vile kaalikwa? Hivi siyo ndio huko Bungeni ambako
tumeona mojawapo ya unyanyasaji mkubwa zaidi wa CDM? Mbowe anayaona au
pia haoni?
Kama Shida ilikuwa ni kupeana mkono na Obama
Sasa
inawezekana Mbowe kama wengine wengi walitaka na kuwa na hamu ya
kupeana mkono na Rais wa Marekani; tena Mweusi “mwenzetu” angalau na wao
wawe na la kusema kuwa tulipeana mkono na Obama au kula naye meza moja.
Hii kweli yaweza kuwa sababu ya kutosha kuvunja kanuni zote za
kupigania haki na kukipaisha chama mbele ya jamii ya kimataifa? Hivi,
keshokutwa serikali hii hii ikimtia pingu tena au ikiwanyanyasa tena
kwenye mikutano kwa kukataa “kutii bila shurti” Mbowe atasimama na
kutaja jina la Kikwete na Serikali kuwa wana matatizo? Really?
Mtu
anaweza kusema ati ujio wa Obama ni suala la kitaifa na halihitaji
siasa? Oh yeah? Hivi CCM na wanachama wake wakianza kujitamba kuwa
Mwenyekiti wao ndani ya uongozi wake ameweza kuwaleta viongozi
mbalimbali wa kimataifa na kupata misaada bwelele watakuwa na makosa;
kwamba na wapinzani nao waliomba sana wawekwe kwenye ratiba kuna watu
watabisha? CCM wana haki zote za kutumia ziara hizi zote kwa kampeni
zao; zinajenga chama na utawala wao madarakani. Sasa kiongozi mkuu wa
upinzani anapobariki anajidhoofisha na kudhoofisha upinzani!
Kama
kweli walikuwa wanataka kukutana na Obama Mbowe na wenzake wajitahidi
kuiondoa CCM madarakani 2015; kwani Obama bado atakuwa na mwaka mmoja
madarakani! Ama wamekata tamaa ya CCM kuondoka madarakani.
Mbowe Aombe Radhi
Ninachopendekeza
ni kuwa Mbowe aombe radhi wanachama wake, mashabiki wake na wengine
ambao wamekwaza na kitendo chake hiki; lakini vile vile aoneshe kuwa
anatambua kinachogombaniwa ni kikubwa zaidi kuliko kujisogeza kwa
watawala. Tayari tumeona kujisogeza kwao wakati wa kwenda Ikulu suala la
Katiba Mpya hakukuwasaidia; kujisogeza kwao na kelele zao zilizuia vipi
Kamuhanda kupandishwa cheo? Si Kikwete huyu huyu amempa IGP Mwema
Nishani ya Utumishi Uliotukuka? Halafu kiongozi wa CDM anaenda na
kuonesha “umoja” na wakandamizaji wake? Hivi kesho kutwa RPC wa Arusha
ambaye amekuwa akimnyanyasa Lema au Mkuu wa Mkoa akipewa vyeo zaidi na
Kikwete Mbowe atasema neno?
Mbowe
kama Mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Upinzani nchini anapaswa kuchora
mstari ambao yeye mwenyewe hatouvuka. Watu wanataka kuona tunaelewa nani
yuko upande gani? Hivi, Mbowe kwa ukaribu wote na Kikwete mbona Kikwete
hadi leo hajaunda tume hata moja ya Kimahakama? Halafu anamwalika Ikulu
anakwenda?
Mbowe
aombe radhi kwa uamuzi wake huu; lakini kama anaona hawezi na kuwa
anataka kuendelea kuwa karibu na Kikwete na serikali yake atafanya jambo
jema sana kuachia ngazi uongozi ili CDM ipate uongozi mwingine ambao
utajua na kusimamia kile inachopigania. Hata kama kwa kufanya hivyo
wataonekana hawaoneshi umoja, heshima, na utaifa mbele ya wageni. Wakati
mwingine mambo mengine yanahitaji kukataliwa tu na kupingwa.
Jambo
pekee ambalo watu huja pamoja bila kujali itikadi, siasa na hata mambo
mengine ni misiba tu. Na hata hapo kuna mistari mingine haivukwi.
Na. M. M. Mwanakijiji
(Picha zote vyanzo mbalimbali)
No comments:
Post a Comment