TTCL

EQUITY

Sunday, April 24, 2016

RAIS MAGUFULI AWASHTUA WENGI,STAILI YAKE YA KUIBUKA MTAAANI YAWAPA HOFU KUBWA

Rais John Pombe Magufuli akiwasalimia walemavu.
 
DAR ES SALAAM: Staili inayotumiwa na Rais John Pombe Magufuli kuibuka katika maeneo mbalimbali mitaani pasipo kutarajiwa, inaonekana kuwashtua wengi huku wengine wakihoji juu ya usalama wake, Risasi Jumamosi linakupa zaidi.
Wakizungumza kwa njia ya simu kutoka maeneo mbalimbali nchini, wananchi wameonesha mshtuko wao, wakisema staili hiyo inaweza kuwapa nafasi maadui zake, waliodai ni wengi, kuweza kumdhuru kwa namna yoyote.
“Unajua utendaji kazi wa Magufuli umempatia maadui wengi na bahati mbaya, wabaya wake ni watu wenye uwezo wa kufanya lolote wakati wowote, sasa anapojitokeza katika maeneo ya wazi bila ya kuwepo ulinzi wa kutosha inatutisha sana, wanaweza kumdhuru hawa mafisadi,” alisema Theo Marson kutoka Arusha.
 
Mwananchi mwingine aliyepiga simu kutoka Morogoro, akijiita Mahsen, alisema ulinzi na usalama wa Magufuli unapaswa kuwa wa hali ya juu, kwani nchi inamhitaji katika mapambano dhidi ya ufisadi, nidhamu na uwajibikaji miongoni mwa watumishi wa umma.

“Hii ibukaibuka yake uswahilini tuna wasiwasi ipo siku wajanja wanaweza kumdhuru, tunamuomba aache, wananchi tusingependa kuona jambo lolote baya linamtokea maana yeye ni mtu muhimu sana kwa Tanzania tunayoitaka, mtusaidie kuziambia mamlaka zinazohusika, ulinzi wake uimarishwe,” alisema Mary Jopel kutoka Mtwara.

Gazeti hili lilijaribu kuwasiliana na Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Grayson Msigwa ili kupata ufafanuzi wa hofu hiyo ya wananchi, lakini baada ya kuomba aandikiwe ujumbe mfupi kupitia simu yake, hakuweza kutoa majibu hadi gazeti hili linakwenda mtamboni.

Tangu kuchaguliwa kwake, Rais Magufuli ameshaibuka sehemu tatu pasipo kutegemewa. Mara ya kwanza ilikuwa ni wakati alipotembelea ofisi za Hazina, akikatisha kwa miguu kutoka ikulu. Pia aliibuka ghafla katika Soko la Kimataifa la Feri jijini Dar es Salaam na kushirikiana na wananchi kufanya usafi.

Katika tukio la karibuni zaidi, wiki iliyopita Rais Magufuli aliibuka katika Tawi la Benki ya CRDB, Holland House, makutano ya mitaa ya Samora na Ohio, jijini Dar es Salaam akiwa katika gari la kiraia bila msafara kama ilivyozoeleka.

No comments:

Post a Comment