TTCL

EQUITY

Thursday, February 18, 2016

Wanavyuo wataka majipu zaidi yatumbuliwe Bodi ya Mikopo.

Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Prof. Joyce Ndalichako.
 
Siku mbili baada ya Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Prof. Joyce Ndalichako, kumfuta kazi Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Mikopo Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB), George Nyatenga, na kuwasimamisha kazi watendaji wengine watatu, uamuzi huo umepokewa kwa furaha na wanafunzi wa vyuo vikuu nchini. 
 
Juzi Prof. Ndalichako alifikia uamuzi wa kumfuta mkurugenzi huyo na kumsimamisha kazi wakurugwenzi watatu wa bodi hiyo kwa tuhuma za ubadhirifu wa zaidi ya Sh. bilioni 3.23 za mikopo ya wanafunzi.
 
Waliosimamishwa ni Mkurugenzi wa Fedha na Utawala, Yusufu Kisare; Mkurugenzi wa Urejeshaji Mikopo, Juma Chagonja na Mkurugenzi wa Upangaji na Utoaji Mikopo, Onesmo Laizer.
 
Ubadhirifu huo ulitokana na mikopo hewa, kulipa waliomaliza vyuo, ambao hawajaomba mikopo huku wengine wakilipwa mara mbili mbili. Hayo yalibainika baada ya mkaguzi mkuu wa ndani kukagua hesabu za bodi hiyo mwaka 2013, lakini mpaka juzi ripoti hiyo ilikuwa imefungiwa kabatini bila kufanyiwa kazi.
 
SOKOINE WAIBUA JIPU LINGINE
Uongozi wa Serikali ya Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (Suaso), umemtaka Waziri Ndalichako kutumbua jipu lingine la watendaji ndani wa Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) kwa kuwa nayo imekuwa kikwazo katika maendeleo ya elimu ya juu, kutokana na kuwakata fedha wanafunzi wakati wa udahili kwa madai ya bima ambayo imekuwa ikilipwa na uongozi wa vyuo.
 
Rais wa Suaso, Francis Ndunguru, alisema uamuzi uliofanywa na waziri huyo ni sahihi kwa kuwa wiki moja iliyopita, walilalamikia bodi hiyo wakidai kuwa watendaji wake wamekuwa kikwazo kwa wanafunzi kupata mikopo.
 
Alisema bodi hiyo ilishindwa kuwapatia mikopo wanafunzi 204 licha ya kutimiza masharti mbalimbali na kulazimika baadhi yao kuahirisha masomo yao, hivyo kuondolewa kwa watendaji hao sasa kutarudisha imani kwa wanafunzi wa elimu ya juu 
Alisema baadhi ya wanafunzi hao ambao wanamaliza muhula wa masomo, mpaka sasa hawajalipwa fedha za kujikimu hata awamu moja, kitu ambacho walishatilia shaka utendaji wa bodi hiyo kabla ya kuondolewa kwa watendaji hao.
 
“Tunamtaka Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), afanye uchunguzi kwa kupitia katika vyuo kwani atabaini madudu mengi yaliyofanywa na watendaji hao waliochukuliwa hatua,“ alisema Ndunguru.
 
Kuhusu TCU, alimshauri Waziri Ndalichako kuitupia jicho taasisi hiyo kutokana na kukusanya fedha kwa kila mwanafunzi kiasi cha Sh. 20,000 ambazo hutokana na fedha zake za kujikimu kwa kisingizio cha bima.
 
USHIRIKA WATAJA KIINI
Rais wa Serikali ya Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Ushirika Moshi (MoCU), Albert Chikira, kwa upande wake, amemtaka Prof. Ndalichako asiishie hapo kwa vile tatizo kubwa liko katika idara inayoshughulika na kumbukumbu za malipo.
 
Chikira alisema kuondolewa kwa viongozi hao kunaweza kuleta ahueni kwa wanafunzi wa vyuo vikuu, kwa vile upatikanaji wa mikopo kwa baadhi yao kulifanywa kama mchezo wa upatu au bahati nasibu.
 
“Utendaji wa HESLB ni tatizo na bado halijaisha. Kinachotakiwa kwa sasa ni kukichunguza kitengo kinachoshughulika na kumbukumbu kwa sababu huko ndiko uchakachuaji wa mikopo na mbinu chafu za kuliibia taifa zinakopikiwa na kufanikiwa. Waziri ni lazima aifumue upya na wahusika wake wachunguzwe kwanza. Tumekuwa tukilalamika mara kadhaa,” alisisitiza.
 
Alisema licha ya uadilifu wa baadhi ya maofisa wa bodi hiyo kutiliwa  shaka kutokana na wizi wa kutisha ulioibuliwa, ni vyema pia Waziri Ndalichako akaigeukia pia TCU, ambayo hudahili wanafunzi ili kubaini kama kuna madudu yanayofanyika kwa wanaojiunga na vyuo hivyo na kupewa mikopo iwapo wana sifa au la.
 
Mwanza wampongeza Ndalichako
Uongozi wa Serikali ya Wanafunzi wa vyuo vikuu vya Mt. Augustino (Saut) na Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) jijini Mwanza, kwa upande wao wamesema hatua aliyochukua Waziri Ndalichako, kutumbua ‘majipu’ HESLB ni ya kupongezwa.
 
Rais wa Serikali ya Wanafunzi wa CBE (Cobeso), Manusura Lusigaliye, alisema walipanga kuandamana kwenda ofisi za HELSB Kanda ya Mwanza kuona namna gani haki zao zinapatikana lakini kutumbuliwa huko kwa watendaji hao wakuu, huenda sasa kero zao zikashughulikiwa.
 
Lusigaliye pia aliwataka wanafunzi wawe wavumilivu kwa kipindi hiki, huku wakiiomba menejimenti ya chuo hicho kuwavumilia wanafunzi ambao hawajapata mikopo yao mpaka sasa. 
 
“Tuna wanafunzi 45 waliotimiza vigezo, lakini hawajapata mikopo  mpaka leo. Pia wapo wengine 22 wa mwaka wa pili ambao hawajapata mikopo tangu wakiwa mwaka wa kwanza,” alisema Antidius Felix, Waziri wa Elimu na Mikopo wa CBE Mwanza.
 
Kwa upande wake, Sogone Mulimi, Rais wa Serikali ya Wanafunzi wa SAUT, aliunga mkono hatua iliyochukuliwa na Waziri Ndalichako, huku akifafanua kuwa huenda uamuzi huo ukaondoa kero kwa wanafunzi na kuwaamsha watendaji wa bodi hiyo kuanza kushughulikia matatizo yao ya mikopo.
 
Hata hivyo, alisema kuna changamoto kwa bodi hiyo kutotoa taarifa kwa wakati kwa wanafunzi wanaoomba mikopo, na kuitaka iboreshe takwimu zake ili kuepusha udanganyifu.
 
UDOM WAFUNGUKA
Rais wa Serikali ya Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), Ezekiel Charb, mbali na kupongeza uamuzi huo, alisema utasaidia kusukwa upya bodi hiyo na kutatua kero zilizojitokeza awali.
 
Alisema bodi ya mikopo imekuwa changamoto kubwa kwa wanafunzi na makosa ya aina hiyo yamekuwa yale yale kipindi chote kama vile fedha kucheleweshwa, wanafunzi kupewa ambao hawana sifa na wengine kupewa wakati hawakuomba kabisa.
 
Alitoa angalizo kwa viongozi walioachiwa mamlaka kwa sasa wasicheleweshe mikopo kwa wanafunzi kwa kuchukua muda mrefu.
 
TAHILISO WAPIGILIA MSUMARI
Kwa upande wake Rais wa Jumuiya ya Taasisi ya Elimu ya Juu nchini (Tahiliso), Stanslaus Kadugalize, alisema wamefurahi kwa uamuzi uliochukuliwa na kwamba umegusa malalamiko yao ya kila wakati yaliyopuuzwa na bodi hiyo.
 
Alisema ilifikia mahali utendaji kazi ndani ya bodi hiyo kuwa wa mazoea zaidi huku wanafunzi wenye shida za msingi wakijibiwa ovyo na watumishi wa bodi.
 
Alisema malalamiko ya wanafunzi wa elimu ya juu, yangeweza kutatuliwa kwa wakati na bodi hiyo lakini ilitawaliwa na kiburi na kuacha kufuatilia na kujifanyia watakavyo.
 
“Bodi ilikuwa na uwezo wa kutatua lakini kwa makusudi waliacha kutekeleza na kuanza kutupiana mpira kati ya bodi na vyuo vikuu huku wanafunzi wakiteseka. Mathalani, mwanafunzi aliyehama chuo chenye ada kubwa na mkopo wake ulishapelekwa, anasumbuliwa kwa makusudi wakati anaweza kutatuliwa tatizo lake, lakini anaelewa kuwa vyuo havijafanya mrejesho,” alisema na kuongeza:
 
"Mwanafunzi huyu ni yatima anategemea mkopo asome lakini tangu mwaka jana hajapewa fedha kwa jambo dogo ambalo ni uhamishaji mkopo wake kutoka chuo kimoja kwenda kingine. Wanatengeneza  mazingira ya kutumia fedha hizo huku masikini wakiteseka. Kuna mengi yalitukera kama wanafunzi lakini kwa kilichofanywa na waziri kitaleta mabadiliko kuna nyota imeaanza kuangaza katika matatizo yetu.".
 
Alisema kwa sasa kuna idadi kubwa ya wanafunzi ambao hawatafanya mitihani kwa kutopewa mikopo, lakini bodi imeshindwa kuangalia mtu mwenye shida bali kujali maslahi yao. 
 
Rais huyo alisema matarajio yao ni makubwa kwa serikali kwa kuwa  tangu serikali ianze kutoa mikopo haijawahi kutokea wanafunzi wa mwaka wa kwanza kupewa zaidi ya asilimia 80, lakini Rais Dk. John Magufuli ameweza.
 
Imeandaliwa na Salome Kitomari (Dar), Ashton Balaigwa (Morogoro), Masyenene Damian (Mwanza), Augusta Njoji, (Dodoma) na Godfrey Mushi (Kilimanjaro).

No comments:

Post a Comment