TTCL

EQUITY

Monday, February 29, 2016

A to Z wapewa siku 7 kulipa faini milioni 70/-

NAIBU Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Luhanga Mpina amewapa siku saba viongozi wa kiwanda cha kutengeneza vyandarua cha A to Z cha hapa kulipa faini ya Sh milioni 70 kilichopigwa na Baraza la Hifadhi ya Mazingira (NEMC) kwa uharibifu wa mazingira.
 
Nemc ilitoa adhabu hiyo Septemba mwaka jana baada ya uongozi wa kiwanda kukutwa na makosa hayo kutokana na uharibifu wa mazingira. Inadaiwa kimekaidi kulipa faini hiyo kwa miezi mitano. Mpina alitoa maagizo hayo baada ya kuzungumza na menejimenti ya kiwanda hicho juzi.
Alisema serikali haiwezi kukubali ukaidi unaofanywa na mwekezaji yeyote kwa sababu yoyote na kwamba wakishindwa kulipa faini hiyo ndani ya siku hizo, kiwanda hicho kitafungwa.
“Hii ni dharau ya hali ya juu na kamwe serikali ya awamu ya tano haiwezi kukubali dharau ya namna hii. Hivyo kwa kuwa mmekiri wenyewe kukiuka sheria kama mlivyoelekezwa na NEMC, hakuna kisingizio chochote ambacho serikali itakubaliana nacho katika hili,” alisema naibu waziri.
Aliendelea kuwaambia, “Kama kweli mna nia njema, badala ya kuendelea kuandika barua za visingizio mngeomba hata kupunguziwa hiyo faini au hata kulipa kwa awamu lakini inaelekea mmeamua makusudi kukaidi maagizo halali ya serikali. Sasa nawapa siku saba mlipe vinginevyo tutakifungia kiwanda.”
Awali, Mkurugenzi Uendeshaji wa Kiwanda hicho, Binesh Haria alijitetea kwamba wameshindwa kulipa faini hiyo kutokana na mawasiliano yanayoendelea kati yao na NEMC kuhusu masharti mbalimbali waliyopewa na baraza hilo katika kuhakikisha mazingira yanakuwa safi na salama.
Hoja hiyo ilipingwa na Mratibu wa NEMC, Kanda ya Kaskazini, Dk Menan Jangu aliyesema tangu kiwanda hicho kilipopigwa faini kimekuwa kikijaribu kukwepa faini hiyo kwa kuandika barua zenye visingizio mbalimbali.
Katika ziara hiyo, Naibu Waziri Mpina alitembelea mfumo wa hifadhi ya maji machafu yanayotumika kiwandani na kuagiza maofisa wa NEMC kufanya ukaguzi wa mara kwa mara kuhakikisha maji hayo yenye sumu hayasababishi madhara kwa wananchi wa maeneo yanayozunguka kiwanda hicho.

No comments:

Post a Comment