TTCL

EQUITY

Saturday, January 30, 2016

HALMASHAURI ARUSHA KUBURUZWA KORTINI.

Mkurugenzi Mtendaji wa jiji la Arusha, Juma Idd
WAFANYABIASHARA jijini hapa wametishia kuiburuza mahakamani Halmashauri ya Jiji la Arusha kwa kuondoa matangazo yao bila notisi kama sheria inavyosema.
Matangazo hayo yanadaiwa kuondolewa katika operesheni ya kuondoa mabango ya biashara ya kampuni kubwa na ndogo jijini Arusha na inadaiwa jiji linayachana, kuyaharibu na kuyang’oa mabango hayo bila utaratibu.
Pia baadhi ya wafanyabiashara hao walilalamikia vitendo vya ubabe pamoja na madai ya kuombwa rushwa na baadhi ya watumishi wa jiji hilo wakati wakiendesha operesheni hiyo na wameiomba Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) iingilie kati.
Desemba mwaka jana na Januari mwaka huu, uongozi wa halmashauri hiyo uliendesha operesheni ya kung’oa mabango ya biashara kwa wadaiwa sugu huku mabango mengine yakichukuliwa na kisha kuhifadhiwa katika viwanja vya jiji hilo.
Mmoja wa wafanyabiashara hao, Riziki Mwalupindi, alisema kwamba baadhi ya watumishi wa jiji hilo wakifuatana na askari Mgambo walifika katika ofisi yake hivi karibuni na kuchana bango lake la biashara bila taarifa yoyote.
Mwalupindi alisema baada ya kitendo hicho alijibiwa ya kwamba wanaendesha operesheni ya wadaiwa sugu wa kodi ya mabango lakini alidai hajawahi kupewa gharama za malipo anayopaswa kulipa. Alidai alipowaomba orodha ya malipo hayo, watumishi hao walimwambia afuatilie katika ofisi za jiji hilo kitendo ambacho alikifanya bila mafanikio yoyote.
“Mimi nimefungua juzi biashara hii, nilienda ofisini kwao kuomba kujua taratibu lakini hawakunipa ushirikiano leo wamekuja kung’oa mabango yangu bila notisi tena kwa ubabe wakiwa na askari,” alisema mfanyabiashara huyo.
Alisema kitendo cha kung’oa mabango yake kimempa hasara ya zaidi ya Sh milioni tano na anawasiliana na mwanasheria wake ili aweze kwenda mahakamani kudai haki yake kwa kuwa hajagoma kulipa kodi hiyo.
Naye mfanyabiashara mwingine, mmiliki wa kampuni ya Skytel, Allbless Shoo, alisema kwamba alilalamikia operesheni hiyo na kudai kwamba baadhi ya watumishi wanaoiendesha, wanaomba rushwa.
Shoo aliliambia gazeti hili kwamba utaratibu huo ni kinyume na sheria kwa kuwa hawajatoa notisi wala orodha ya gharama za malipo kwa wadaiwa na kusema kwamba watakwenda mahakamani kudai haki zao.
Akijibu madai hayo Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Arusha, Juma Idd, alisema kwamba kwa sasa bado anawasiliana na wanasheria wa jiji hilo kwa lengo la kutaka ufafanuzi na akishapata taarifa kamili atawaita waandishi wa habari kutolea ufafanuzi.
 CHANZO ; HABARI LEO.

No comments:

Post a Comment