TTCL

EQUITY

Friday, December 25, 2015

Uokotaji chupa, ajira ya kipato inayodhaniwa ni ya maamuma

Mjasiriamali Daniel Julias, akikagua mzigo uliofikishwa katika eneo lake la biashara, kwa ajili ya kuupima.
 
Kuna kasumba dhidi ya biashara ndogo zikionekana hazina maana na zinadharauliwa, ingawa uk0weli upo katika upande wa pili kwamba, kwa kiasi kikubwa zinainua maisha ya baadhi ya watu kiuchumi.
 
Moja ya maeneo hayo ni ujasiriamali wa kuokota na kuuza chupa za plastiki jijini Dar es salaam, ambao watu wengi hawajaupa nafasi katika kubadilisha maisha ya wengi katika maendeleo.
 
Hilo limejidhihirisha kwa maisha ya kijana, Daniel Julias, anayejishughulisha na ujasiriamali wa kuokota na kuuza chupa za plastiki jijini Dar es salaam.
 
Julias anasema, biashara hiyo imemsaidia kuhudumia familia yake aliyoiacha kijijini kwao alikotaja ni mkoani Tanga, hata akafanikiwa kununua tofali kwa ajili ya ujenzi, huku akiwasaidia wazazi wake kuendesha kilimo.
 
 “Mimi nilivyokuja Dar es Salaam, nilihangaika sana kutafuta maisha, lakini namshukuru Mungu, kwani ujasiriamali huu unanipatia kipato ambacho kinanisaidia mimi na familia yangu iliyopo kijijini,” anasema Julias.
 
Anasema, imezoeleka kwa baadhi ya watu wanapoonekana kuokota chupa jalalani na barabarani, wanahisiwa wamechanganyikiwa au wahuni, dai analolipinga kwa kila namna.
 
Julias anajigamba, hiyo ni biashara inayowaingizia kipato kikubwa na wakati mwingine katika kiwango cha kuwazidi waajiriwa.
 
Julias, mkazi wa Keko jijini Dar es Salaam, ambaye shughuli zake za kuokota na kuuza chupa anaziendesha katika eneo la Kimara Baruti, anasema katika kazi hiyo wapo watu anaowaita ‘wasiojitambua.
 
Anawatafsiri watu hao kuwa wanatafuta fedha za kwenda kunywa pombe na kutumia dawa za kulevya kupitia biashara ya ukusanyaji chupa, lakini katika sura ya pili, wapo wanaojitambua na wamefanikiwa kimaisha.
 
HOFU YA DHARAU
Anasema, waokota na wauza chupa za palstiki wengi, hawafanyi hivyo katika maeneo wanayoishi, kwa kuhofia kuchekwa na kudharauliwa, kutokana na jamii kukosa uelewa sahihi kuhusu kazi hiyo.
 
Tino Fantaeli, ambaye ni mfanyabiashara wa kuokota na kuuza chupa na mkazi wa Makumbusho Kijitonyama, jijini Dar es Salaam, anayefanya biashara zake eneo la Kimara Baruti, anaeleza:
 
“Mimi nikiondoka nyumbani kwangu, watu wanajua nafanya kazi katika ofisi ya maana, kwani nakuwa nimevaa vizuri, tofauti na hivi unavyoniona.” 
 
Anaeleza kuwa, kutokana na tabia hiyo ya jamii kuwadharau, wamekuwa wakifanya biashara hiyo wakitawaliwa na hofu ya kuchekwa na kudharauliwa.
 
Julias anafafanua kuwa, jamii inapaswa kufahamu kuwa, mbali na kuokota chupa na kuuza, pia ni wadau bora wa kusafisha mazingira kwa kuokota chupa zinazozagaa kama takataka.
 
GHARAMA ZA CHUPA
 Anasema, mtu anayefanya biashara hiyo na anajituma ipasavyo, anaweza kutanua wigo wao wa kipato.
 
“Sikudanganyi, mtu akijitahidi na akiwa na malengo, anaweza kuingiza hata zaidi ya sh.60, 000 kwa siku, kwani kwa siku tunauza mara tatu; asubuhi, mchana na jioni. Sasa hapo mtu akijitahidi anafikia malengo,” anajigamba Julias.
 
Anaongeza kuwa, huwa wanauza kilo moja ya chupa za plastiki kwa bei ya sh. 200, mifuko ya pkastiki sh.150 na ndoo zilizoharibika sh.300.
 
Julias anaongeza kuwa, baada ya kuwauiza wanunuzi wao ambao huwa wanaenda kuziuza chupa hizo katika viwanda vikubwa katika maeneo ya Tegeta, Mwenge, Kurasini na Mbagala, ambako huwauzia raia wa kigeni anaowataja kuwa Wachina, kwa bei ya kati ya sh. 450 hadi 500 kwa kilo.
 
Anasema, wafanyabiashara wenye mitaji mikubwa, mara nyingi huingia kwenye masoko makubwa ya chupa na kupeleka katika mikoa kama vile Morogoro na nchi jirani ya Kenya, zinakochukuliwa kama malighafi ya viwandani na kuyeyushwa ili kutumiwa tena. 
 
FAIDA ALIZOPATA 
Akieleza faida anazozipata tangu aanze biashara hiyo kwa muda wa miaka miwili, anataja ni pamoja na kumsaidia kulipa kodi ya nyumba anayoishi na kuwasaidia wazazi wake waliopo kijijini.
 
“Unajua Dar es Salaam sio kwetu, hivyo ninavyopata fedha, naangalia kuwekeza nyumbani, kwani hivi sasa nimenunua matofali kwa ajili ya kujenga nyumba yangu na huwa nawasaidia wazazi wangu kulipia wafanyakazi wa shambani katika msimu wa kilimo,” anasema.
 
Katika eneo la Mwenge Mlalakuwa jijini Dar es Salaam, mwandishi wa makala hii alikutana na mwanamke mzee aliyejitambulisha kwa jina la Maria Mwangosongo (87), akiwa amebeba mzigo mgongoni uliokuwa na chupa za plastiki.
 
Bibi huyo anaeleza, kwa kawaida anazipeleka chupa hizo ili kuziuza, apate fedha za kujikimu kimaisha, yeye na wajukuu wake wanaoishi pamoja.
 
“Mimi ni mjasiriamali, mjukuu wangu hizi chupa nilishinda jana huku naokota mitaani, hapa nikienda kuuza najipatia fedha na kwenda kununua chakula nile na wadogo zako (wajukuu wake)nyumbani,” anajieleza mwanamke huyo mzee.
 
Anasema, kazi hiyo ya kuokota na kuuza chupa za plastiki, aliianza baada ya kubaini hana msaada kutoka kwa ndugu na watoto wake, waliomwachia watoto zao, pasipo kumwelekezea kipato chochote.
 
“Mimi ni mjasiriamali mjukuu wangu. Hizi chupa nilishinda jana huku naokota mitaani hapa, nikienda kuuza najipatia fedha na kwenda kununua chakula nile na wadogo zako nyumbani (wajukuu wake),” anasema.
 
Anafafanua, amekuwa akipata changamoto wakati wa kuokota chupa, kwani mara nyingi wanapenda kwenda jalalani sehemu za starehe, kwani huko ndiko kuna watumiaji wa vinywaji vya plastiki.
 
Bibi huyo naye anajigamba kuwa, biashara hiyo imesaidia kuweka mazingira ya jiji la Dar es Salaam safi na kuyatunza, kwani iwapo kusingekuwepo, wafanyabishara wanaonunua chupa, jiji lingebaki chafu.
 
DHANA POTOFU
Hata hivyo, wakati kuna kundi la wafanyabishara wa kuokota na kuuza chupa za plastiki jijini, bado katika jamii kuna dhana potofu inayowahusu.
 
Mjasiriamali aliyejitambulisha kwa jina moja la ‘Mangi’ wa eneo la Kimara, jijini Dar es Salaam, anasema watu anaowatafsiri ni wafanyabiashara hiyo, kumbe katika uhalisia ama wana matatizo ya akili au walevi wa pombe kupindukia.
 
Anasema, jambo linalomkatisha tamaa mara nyingi ni kitendo cha baadhi ya watu katika jamii kumdharau pale anapoonekana akiokota chupa, kununua na hata kuzibeba katika maeneo mbalimbali ya jiji. 
 
“Wengi wakiniona naokota chupa, wanadhani mimi ‘Chizi’. Huwa nachukia sana, kwani sina uwezo wa kuwabadilisha mtazamo wao,” anasema.
 
Anakiri, kuna kundi la anaowaita ‘mateja’ kwa maana ya watumiaji wa dawa za kulevya, wanaofanya kazi hiyo, ndio  ambao mara nyingi wanawaharibia sifa zao.
 
Julias anaeleza kuwa, jamii inapaswa iwatambue na kuwathamini wanaokusanya makopo, kama wanaharakati wa utunzaji wa mazingira.

No comments:

Post a Comment