Na Aidan Mhando,Mwananchi
Dar es Salaam. Hali ya usafiri
kwenye kituo kikuu cha mabasi yaendayo mikoani na nchi jirani cha Ubungo
(UBT) ni mbaya hasa kwa mabasi yanayokwenda Kilimanjaro na Arusha.
Hali hiyo imesababisha Mamlaka ya Usafiri wa Nchi
Kavu na Majini (Sumatra), kuruhusu mabasi madogo aina ya ‘Coaster’
kusafirisha abiria wanaokwenda mikoa hiyo.
Pamoja Sumatra kuruhusu magari hayo kusafirisha
abiria kwenda mikoa hiyo, kumeibuka malalamiko kutoka kwa baadhi ya
abiria wakidai kutozwa nauli kubwa kuliko iliyoelekezwa.
Abiria wanadai kutozwa kati ya Sh35,000 hadi 40,000 badala ya Sh20,000 hadi 25,000 kwa mtu mmoja.
Mwananchi ilishuhudia umati wa abiria kituoni hapo
asubuhi ya jana, huku kukiwa na habari zisizo rasmi kuwa kuna mgomo
baridi kwa baadhi ya mabasi baada ya kubanwa kutopandisha nauli.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti abiria hao walidai kuwa hali ya usafiri UBT ni mbaya kutokana na uhaba wa mabasi.
Moja ya abiria Joseph Masawe, aliyepanga kusafiri
kwenda Kilimanjaro alisema: “Bora waandishi mmefika mjionee wenyewe hali
mbaya ya hapa Ubungo. Abiria ni wengi na mabasi hakuna.”
Aliongeza: “Pamoja na shida hii ya usafiri, bado
tunapandishiwa nauli kupita kiasi. Ukitaka kuigusa Coaster lazima uwe na
Sh35,000 au Sh40,000.”
Abiria mwingine Emmanuel Musa alisema: “Tunahisi
huenda kukawa na mgomo baridi baada ya wenye mabasi kutakiwa
kutopandisha nauli, kwani tunashangaa hakuna mabasi ya Arusha na
Kilimanjaro.” Akizungumzia suala hilo Ofisa Leseni anayeshughulika na
ukaguzi wa mabasi kituoni hapo, Sebastian Lohay alisema kutokana na
wingi wa abiria wametoa vibali kwa wenye ‘Coaster’ kusafirisha abiria
kwenda Mikoa ya Kaskazini.
“Ni kwamba abiria wengi na mabasi ni machache,
lakini hakuna mgomo baridi,” alisema Lohay alipoulizwa kama kukosekana
mabasi hayo ni kutokana na kuwepo kwa mgomo baridi.
Kuhusu kupandishwa kwa nauli, alisema: “Ni kweli
kuna baadhi ya mabasi madogo Coaster yamekuwa yakitoza nauli tofauti na
iliyoelekezwa, na wanaofanya hivyo tukiwabaini tunawakamata na kuwatoza
faini.”
Naye Ofisa wa Chama Cha Kutetea abiria (Chakua),
Gervas Rutaguzinda alisema watu wenye mabasi madogo wamekuwa
wakipandisha nauli na kuwataka abiria kutotoa taarifa.“Hali ni mbaya, nauli zipo juu abiria wamekuwa wakilalamika, lakini cha
kusikitisha ni kwamba hawa wenye mabasi wanawatisha abiria kuwa wakitoa
taarifa za kupanda kwa nauli watasitisha safari zao,”alisema.
No comments:
Post a Comment