RAIS KIKWETE APELEKEWA BARUA YA KULIVUNJA BUNGE MAALUM LA KATIBA
Mwenyekiti wa Bunge la Katiba,Samuel Sitta
Dodoma. Ombi la Mjumbe wa Bunge la Katiba, Mchungaji Christopher la kutaka Bunge hilo livunjwe, limekuwa zito kwa Mwenyekiti Samuel Sitta.
Kutokana na ugumu huo, Sitta amelazimika kumpatia barua Mtikila ili
awasilishe hoja yake kwa Rais Jakaya Kikwete, ambaye kisheria ana
mamlaka hayo ya kuvunja Bunge la Katiba, ambalo limekuwa likionekana
kwenda mrama.
Mtikila, ambaye ni mwenyekiti wa Chama cha Kidemokrasia na mjumbe wa
Bunge la Katiba aliwasilisha barua yenye hoja binafsi akitaka bunge hilo
livunjwe na wajumbe warejee makwao kwa madai kuwa chombo hicho cha
kutunga Katiba mpya hakijali maslahi ya umma na uongozi umekuwa
haumtendei haki.
Majibu ya barua hiyo yalikuwa hivi: “Nimeagizwa na Mwenyekiti wa Bunge
Maalumu nikujulishe kwamba Bunge Maalumu halina uwezo wala mamlaka ya
kujitangaza kwamba ni haramu na hivyo livunjwe ; na kwamba hoja hiyo
haistahili kuwa hoja ya Bunge Maalumu,” inasomeka barua hiyo
iliyoandikwa na katibu wa Bunge hilo, Yahya Khamis Hamad.
Akizungumza na Mwananchi jana, Sitta alikiri kumpatia barua hiyo Mtikila
ili aende kwa Rais Kikwete kwa sababu hoja yake kutaka kuvunjwa Bunge
haiwezi kusikilizwa na chombo hicho kwa kuwa mwenye madaraka ya kuvunja
Bunge ni Rais pekee.
“Ni kweli ametuletea hoja ya kuvunja Bunge. Ameandika mambo mengi,
akitumia lugha ya uchochezi, kama kudai kwamba ‘Tanganyika imekuwa
koloni la Zanzibar kwa muda mrefu’, lugha ya namna hii hatuwezi
kuikubali,” alisema Sitta.
No comments:
Post a Comment