TTCL

EQUITY

Tuesday, December 3, 2013

IGP MWEMA UNAOMBWA UTEMBELEE…CHINJACHINJA STREET ILIYOPO UKONGA WATU WANAUAWA SANA

 
INAPOFIKIA nyakati ambazo watu wanafanya vitendo hatari utafikiri hakuna serikali, athari yake huwa ni kubwa zaidi. Matokeo mabaya ni wananchi kujichukulia sheria mkononi na kusababisha hata wasio na hatia kuuawa kinyama. 
 
Inspekta Jenerali wa Jeshi la Polisi Tanzania (IGP), Said Mwema.
Kabla ya kwenda mbali labda yapo maswali ya kujiuliza; Kwa nini mtu atoe uhai wa mwenzake kwa mtindo wa rejareja? Mbona wauaji hawakamatwi? Nini kinasababisha unyama huo haukomeshwi? Jeshi la polisi jukumu lake ni nini?
Ni muda mwafaka kwa Inspekta Jenerali wa Jeshi la Polisi Tanzania (IGP), Said Mwema, kusikia kilio cha Watanzania ambao wanapoteza ndugu zao, wengine wanajeruhiwa, huku mamia wakiishi roho mkononi kwa hofu.
Mtaa wa Ukonga Mazizini ndiyo Chinjachinja Street, kikundi hatari kimeweka kambi eneo hilo, kazi kuu ni kufanya uporaji wa kutumia mapanga na nondo. Wanaua watu kikatili. Kinachoshangaza ni kwamba mtaa huo upo Wilaya ya Ilala, ndani ya Kanda Maalum ya Dar es Salaam.
HATARI ILIYOPO
Uchunguzi umebaini kuwa ndani ya Oktoba peke yake, Watanzania nane wameuawa katika mtaa huo. Hiyo ni wastani wa watu wawili kwa kila wiki.
Hali hiyo, imesababisha kilio cha wakazi wa eneo hilo, kwani wamekuwa hawawezi kufanya mizunguko kuanzia saa 1 usiku kwa hofu ya kukabwa, kupigwa mapanga na kuuawa.
“Giza linapoingia tu, hakuna mtu anaweza kukatiza mtaa huu, inabidi kujifungia ndani maana ukitoka tu unageuzwa bucha, utapigwa mapanga na nondo, ukinusurika kuuawa heri yako,” alisema Liadi  Kimaro, mkazi wa mtaa huo na kuongeza:
“Wakati mwingine ikitokea umemaliza shughuli zako usiku, inabidi upige simu nyumbani kuitaarifu familia kisha unalala hoteli, maana kurudi nyumbani ni kuhatarisha maisha.
“Kuna kipindi hali inakuwa mbaya hata mchana, kuna watu walipigwa mapanga na kuuawa wakati bado kweupe kabisa. Tuna kituo cha polisi lakini hawazuii unyama huu.”

HAWA WAMESHAUAWA
Wafuatao, wamebaki majina tu, wao walishatangulia mbele za haki, waliowakatisha uhai ni watu hao hatari ambao waliwaua kinyama.
Emmanuel Marwa aliuawa Oktoba 2 (saa 4 usiku), James Kitoma, Oktoba 5 (saa 2 usiku), Siwema Abdul, Oktoba 11 (saa 12 jioni), Samson Bernard, Oktoba 15 (saa 5 usiku) na Manyati Wiliam, Oktoba 20 (saa 3:30 usiku).
Wengine ni Maneno Yohana, Oktoba 23 (saa 5 usiku), Ramadhani Athumani, Oktoba 29 (Saa 5 usiku), Jumbe Saadam, Oktoba 30 (saa 2 usiku).
Hata hivyo, zipo taarifa kwamba wengine watatu waliuawa katika mwezi huo lakini Uwazi halijaweza kuthibitisha madai hayo.
Waliouawa Septemba mwaka huu ni Noel Karoto, Septemba13 (saa 11 alasiri), Daudi John, Septemba 14 (saa 3 usiku), Herrieth Ishengoma, Septemba 23 (saa 1:45 usiku), Zawadi Bwera, Septemba 28 (saa 3 usiku) na Jacob Simba, Septemba 29 (saa 2:20 usiku).
WALIONUSURIKA KIFO
Mwandishi Mwandamizi wa Uwazi, Haruni Sanchawa ni mmoja wa waathirika wa unyama unaotendeka kwenye eneo hilo, kwani alivamiwa Oktoba 12, mwaka huu, akiwa anatokea kazini kurejea nyumbani kwake.
Sanchawa ambaye anaishi mtaa huo, alipigwa nondo na bisibisi na kujeruhiwa vibaya sana, ingawa kwa kudura za Mwenyezi Mungu aliweza kupona baada ya madaktari kufanya kazi nzuri ya kupigania uhai wake.
Wengine ambao waliwahi kuvamiwa na kuachwa majeruhi ni Emmamuel Goigoi, aliyecharangwa mapanga Oktoba 6 (saa 5 usiku), Paulo Julius, Septemba 2 (saa 5 usiku), Abdallah Yusuf, Septemba 4 (saa 2 usiku), Thomas John, Oktoba 7 (saa 6 usiku) na Aisha Mohamed, Septemba 8, (saa 12 asubuhi).
HII NI KUSEMA DAR SIYO SALAMA
Aliyekuwa mjumbe wa Tume ya Katiba, marehemu Dk. Sengondo Mvungi, alifikwa na mauti kutokana na kuvamiwa na waporaji ambao walimpiga mapanga na kumjeruhi vibaya kabla ya kufikwa na mauti nchini Afrika Kusini alikopelekwa kwa matibabu.
Hivi karibuni, yalitokea mauaji ya watu watatu maeneo ya Goba Darajani na Kimara Suka, Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam, chanzo cha vifo ni ujambazi wa kutumia mapanga, nondo na bisibisi.
Matukio hayo na mengine mengi yanayoendelea kutikisa jiji, ukiyaweka kwenye kapu moja, jawabu la jumla ni kwamba Dar es Salaam siyo salama.
AJABU KUHUSU DOLA
Eneo la Ukonga Mazizini, limekuwa linashangaza wengi kwa sababu limezungukwa vikosi vya usalama kiasi kwamba kwa akili ya kawaida, siyo rahisi kuamini kama matukio hayo yanaweza kutokea.
Ukonga Mazizini ni jirani na kambi ya askari polisi wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), Jeshi la Magereza na Jeshi la Wananchi, Kikosi cha Anga (Air Wing) na cha Gongo la Mboto, vikosi hivyo vyote vinapakana na eneo hilo hatarishi kwa maisha ya Watanzania.
“Mtu ukipewa ramani ya Ukonga Mazizini, unaweza kudhani ni eneo salama zaidi la kuishi kwa sababu lipo jirani na kambi za vikosi vya usalama lakini nashangaa sijui hao waporaji wanapata wapi kiburi, maana hawaogopi,” alisema Job Lembeli, mkazi wa eneo hilo.
WANANCHI WALISHAKATA TAMAA
Kuonesha kwamba wamekata tamaa, hivi karibuni wananchi ambao ni wakazi wa Ukonga Mazizini, waliamua kuandamana mpaka Kituo Kidogo cha Polisi cha Mazizini na kutishia kukichoma moto kwa madai kwamba hakiwasaidii. Wakiwa na hasira kali, wakazi hao waliwatuhumu baadhi ya askari polisi wa kituo hicho kuwa wanaendekeza rushwa badala ya kuwaokoa raia wanaoteseka kwa mashambulizi ya majambazi wauaji.
“Tukifika kituoni kuomba mtuhumiwa akamatwe, tunaombwa shilingi 20,000 mpaka 30,000 ndipo wachukue maelezo yako na kwenda kumkamata mtuhumiwa,” alisema mmoja wa wananchi akiwa kituoni hapo, huku wengine wakidai:
“Tunateswa na mateja (watumia madawa ya kulevya), polisi wanawajua lakini hawawakamati, kuna mchezo hapa, watu wanakufa, polisi wanaangalia tu.”
Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Mazizini, Joseph Alexander Kabati, alipoulizwa kuhusiana na uhalifu eneo hilo, alikiri kisha akasema:“Wananchi ni wabishi, hawataki ulinzi shirikishi, wakiambiwa wachangie fedha ili vijana wajitolee kulinda hawataki.”
-Global publishers

No comments:

Post a Comment