TTCL

EQUITY

Wednesday, March 23, 2016

Mbunge Vicky Kamata Afunga Ndoa na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Dk. Likwelile

Mbunge wa Viti Maalamu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Vicky Kamata amefunga ndoa na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Dk Servacius Likwelile.
Dk Likwelile amefunga ndoa hiyo baada ya mkewe wa awali kufariki dunia Mei mwaka 2014.

Kwa hatua hiyo, Dk Likwelile amemfuta machozi mbunge huyo kijana baada ya ndoa yake ya awali aliyotarajia kuifunga na Charles Pai kukwama dakika za mwisho wakati wa maandalizi yote ya msingi kukamilika.
 
Dk. Likwelile
Habari ambazo Tanzania Daima imezipata, zilieleza kwamba mbunge huyo ambaye ni msanii wa muziki wa kizazi kipya , alifunga ndoa hiyo Septemba mwaka jana katika ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Geita.
Habari zinaeleza kuwa wawili hao baada ya kufunga ndoa, hawakuwa na sherehe kubwa bali walikuwa na ‘pati mchapalo’ iliyofanyika nyumbani kwa Dk Likwelile na kuwashirikisha baadhi ya wana ndugu na marafiki wa pande zote mbili.

“Wamefunga ndoa bomani, hakukuwa na sherehe bali kulikuwa na hafla ndogo iliyofanyika nyumbani na wanafamilia wachache ndio walioshiriki,” alisema mtoa habari wetu ambaye alikuwa mmoja wa watu wachache walioshuhudia ndoa hiyo.

Alipotafutwa kwa njia ya simu kuthibitisha taarifa hizi, Kamata alikiri kufunga ndoa hiyo, lakini hakuwa tayari kuzungumza zaidi.

“Umepata wapi hizi taarifa? Ila ni kweli nimefunga ndoa, ninachojua ni kwamba Dokta Likwelile ni mume wangu halali, namshukuru Mungu kwa hilo,” alisema kwa kifupi Vick na kukata simu.

Mei 24 mwaka 2014, Vick Kamata alikwama kufunga ndoa na Charles Pai baada ya kubainika kuwapo kwa kasoro kwenye nyaraka za mwanaume.

Hali hiyo ilisababisha mbunge kuugua ghafla kutokana na mshituko alioupata na kulazimika kulazwa katika Hospitali ya Tabata Genaral iliyopo Segerea. Ndoa hiyo ilikuwa ifungwe katika Kanisa Katoliki Parokia ya Bikira Maria Mama wa Mkombozi, Sinza jijini Dar es Salaam na tayari kadi za mialiko zilikuwa zimesambazwa kwa watu mbalimbali wakiwamo wabunge.

Kamata ni msanii wa muziki aliyetamba na kibao chake cha “ Wanawake na Maendeleo” na pia ni mtetezi wa haki za wanawake.

No comments:

Post a Comment