TTCL

EQUITY

Thursday, December 3, 2015

Tazara nako ni mshikemshike



KASI ya utendaji kazi katika Serikali ya Rais Dkt. John Magufuli, imehamia Shirika la Reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA), baada ya Serikali kuagiza Menejimenti ya shirika hilo kuanza kujitegemea ifikapo Juni, mwakani kuhakikisha inalipa watumishi wake mishahara.
Serikali imesisitiza kwamba haitaendelea kubeba mzigo wa kulipa wafanyakazi wa Tazara mishahara ifikapo mwezi huo.
Agizo hilo lilitolewa na Katibu Mkuu Wizara ya Uchukuzi Dkt.Shaaban Mwinjaka, wakati wa hafla ya kukabidhi mabehewa 18 na vichwa vinne kwa ajili ya reli ya Tanzania kutoka nchini China, vyenye thamani ya dola za Marekani mil 22.4.
Lengo la msaada huo ni kuendeleza mahusiano mazuri ya nchi tatu za Tanzania, Zambia na China.
Alisema kuwa,serikali haitaendelea kuibeba Mamlaka hiyo kwa kuwalipa watumishi wake mishahara na badala yake itumie fursa zilizopo kusimama yenyewe.
"Upatikanaji wa mabehewa haya kutoka serikali ya China ni moja ya fursa itakayowezesha TAZARA kusimama, Viongozi wa Menejiment tumieni fursa zilizopo kuhakikisha mnasimama imara, kwani Serikali mpaka kufikia Juni 2016 haitabeba jukumu la kuwalipa watumishi wenu mishahara,"alisema Dkt. Mwinjaka.
Aliitaka Mamlaka hiyo kuhakikisha inafanya kazi kwa kasi inayoendana na rais wa sasa ya 'Hapa Kazi Tu' na kuhakikisha inafikia malengo yaliyowekwa na reli hiyo tangu enzi za rais wa awamu ya kwanza kwa kubeba tani mil 5 kwa mwaka.
"Inasikitisha sana kuona TAZARA ikiwa hoi hadi na kufikia kubeba tani 87,000 kwa mwaka wakati lengo likiwa ni kubeba tani milioni tano,",alisema na kuitaka Menejimenti ya Tazara kukimbia mchakamchaka ili kuondokana na hali hiyo.
Aidha aliitaka Tazara kufanya mabadiliko ya uongozi ili kuweza kuboresha utendaji kazi huku akisisitiza kuwa Tanzania na Zambia bado ziko tayari kuendelea na mashirikiano katika sekta hiyo ya uchukuzi ili kuweza kufikia malengo.
Hata hivyo Balozi wa Zambia nchini, Judith Kapijimpanga, alisema ushirikiano wa nchi hizo ulianza tangu zamani na kwamba lengo kubwa likiwa ni kuimarisha sekta ya uchukuzi.
Alisema mbali na kuimarisha sekta hiyo pia imewezesha kurahisisha usafiri wa reli hasa kwa watu wa hali ya chini, kwani treni hizo zimekuwa zikifanya safari kutoka Tanzania hadi Zambia.
Naye mwakilishi kutoka Serikali ya China, Zhao Zhongning, alisema kuwa,serikali ya china itaendelea na mashirikiano na Tanzania kwa kuzingatia taratibu zinazokubalika.
Alisema kuwa kwa miaka mingi nchi hiyo imekuwa ikishirikiana katika shughuli mbalimbali za kimaendeleo hususan uchukuzi na kwamba ndiyo nchi iliyojenga reli hiyo tangu enzi za rais wa awamu ya kwanza.
Wafanyakazi Tazara walilalamikia menejimenti kwa kushindwa kusimamia ufanisi wa kazi huku wakimuomba rais Dkt. Magufuli kufanya ziara ya kushtukiza ili kujionea madudu yanafanyika ikiwemo kuwachukulia hatua zaidi viongozi wao. 

No comments:

Post a Comment